MAAFISA wawili wakuu wa Serikali katika kaunti ya Nyeri, jana walilazimika kuacha sherehe za siku kuu ya mashujaa na shughuli zao zingine za kikazi ili kuhudhuria mazishi ya mkazi aliyewaagiza wasikose kuhudhuria mazishi yake kabla ya kujinyonga.
Naibu kamishna wa wilaya ya
Tetu Bw Haman Shambi na kamanda wa polisi wa utawala Bw Wilfred Chacha,
walisema walifahamishwa kwamba John King’ori aliacha ujumbe akiwaagiza
lazima wahudhurie mazishi yake.
Bw King’ori alijinyonga siku
chache zilizopita nje ya nyumba yake katika lokesheni ya Hu-hoini
kaunti ya Nyeri na kuacha ujumbe huo uliopatikana na maafisa wa polisi
waliochunguza kifo chake.
Bw Shambi na Bw Chacha walishtushwa na agizo la marehemu la kuwataka wasikose kuhudhuria mazishi yake.
“Nilishtuka kwa sababu sijawahi kualikwa na marehemu maishani mwangu nihudhurie mazishi yake,” akasema Bw Shambi.
Maafisa hao wawili walikuwa wanamfahamu Bw King’ori alipokuwa mfanyakazi wa afisi za Hazina ya eneo Bunge la Tetu (CDF).
Walikiri kwamba hawakufahamu
kwa nini aliandika ujumbe huo na kuongeza kwamba angesema sababu ya
kuwataka wafike kwenye mazishi yake.
“Kulingana na desturi za
Kiafrika, sio kawaida kupuuza ombi la marehemu, kwa hivyo nilifika ili
kuepuka laana. Hata hivyo, ninashangaa kwa nini alitaka nihudhurie
mazishi yake,” akasema Bw Chacha.
Maafisa hao walisema walilazimika kuacha shughuli zao ili kutoa heshima za mwisho kwa marehemu.
“ Nilipasa kuchunguza kesi
ya wizi wa mitambo ya stima lakini nikamtuma naibu wangu ili niitikie
wito wa marehemu,” akasema Bw Chacha.
Alieleza kwamba awali marehemu alijaribu kujinyonga lakini familia yake ikamzuia.
“Kujaribu kujitoa uhai ni
tendo la uhalifu na pengine angekuwa hai kama familia yake ingeripoti
kwa polisi kwa sababu tunapowakamata wanaojaribu kujinyonga, tunawapa
ushauri nasaha,” akasema.
Bw Shambi alisema marehemu alikuwa na shida tangu afutwe kazi katika ofisi za CDF.
“Binafsi nilimsaidia na
magunia ya mahindi na maharagwe lakini sikuweza kumsaidia kupata kazi
tena katika afisi za CDF kwa sababu kipindi chake kilikamilika,” akasema
na kuwataka wakazi wawasaidie wenzao walio na shida.
Chifu wa eneo hilo Duncan
Mureithi alisema marehemu alikuwa mtu mchangamfu aliyekuwa akitoa habari
kwa wakazi kuhusu matukio muhimu.
Hata hivyo, aliongeza kwamba alikuwa akigombana na mkewe kila wakati.
Chifu huyo alisema kabla ya kujinyonga, mkewe alitembelea ofisi yake kutafuta ushauri kuhusu ndoa yao.
“Mke wangu alikuja kwa afisi
yangu kutafuta ushauri wa jinsi ya kutatua mzozo wa ndoa yao, lakini
mumewe alikataa kufika na kuamua kuzungumza kwa simu kusuluhisha mzozo
huo,” akasema Bw Mureithi.
Aliongeza kwamba marehemu alikuwa na watoto watatu na kifungua mimba alikuwa shule ya upili.