Watu wawili wanaodhaniwa kuwa ni majambazi wakiwa na bunduki aina ya SMG na bastola waliokuwa wakitumia pikipiki aina ya Sanlg yenye namba T460 CVQ wamevamia duka la Mpesa na kumuua mfanyabiashara Gosbert Kulwa(59) mkazi wa Tambukaleli mjini Geita.
Kamanda
wa polisi mkoani Geita Joseph Konyo amesema tukio hilo limetokea jana
majira ya saa 11.30 jioni katika eneo la benki ya NMB ambapo majambazi
hao walimpiga risasi ya tumboni mfanyabiashara huyo wa Mpesa na kufariki
dunia wakati akipata matibabu katika hospitali ya wilaya ya Geita.
Amesema
mauaji hayo yalifanyika baada ya majambazi hao kupora kiasi cha pesa
ambacho hakijajulikana kutoka kwa mfanyabiashara huyo wa Mpesa.
Kamanda
ameongeza kuwa kabla hawajamuua Gosbert walianzia kwenye duka la
mfanyabiashara wa vinywaji ndugu Ignas Athanas na walichukua pesa kiasi
cha shilingi millioni moja na laki nane na kumpora bastola aina ya H
PIETRO BERRETA HO4788Y CAR 5808 ikiwa na risasi 12 mali ya
mfanyabiashara huyo.
Aidha
majambazi hao walikuwa na bunduki aina ya SMG iliyofutwa namba zake na
risasi 13 na simu ya mkononi aina ya TECNO huku wakiwa wamevalia makoti
meusi na helment ili kuficha sura zao zisitambulike kwa urahisi.
Jeshi
la polisi lilipata taarifa muda mfupi ambazo zilizotolewa na raia
wema ambapo kamanda wa polisi akiongoza kuwafuatilia majambazi hao
walifanikiwa kuwakuta katika pori lililopo jirani na kijiji cha Ibambila
wilayani Nyangh’hwale zaidi ya km 50 kutoka mjini Geita walipofanya
uharifu.
Wakiwa
wanakimbizana, majambazi hao walipowaona askari, jambazi mmoja
aliyekuwa na silaha aliruka kwenye pikipiki na kuanza kuwashambulia
askari kwa risasi lakini dereva wa polisi alimfuata moja kwa moja na
kumgonga kwa gari jambazi huyo na kufariki papo hapo.
Baada
ya hapo jambazi mwingine alikimbia kwa pikipiki na askari wakaanza
kumfukuza wakishirikiana na wanafunzi wa shule ya sekondari Nyang’hwale
na kufanikiwa kumkamata na kuanza kumshambulia na alifariki wakati
anakimbizwa hospitali.
Taharuki hiyo iliukumba mji wa Geita kwa masaa takribani 3 kabala hawajakamatwa majira ya saa 2 .
Baadhi
ya wananchi wamelipongeza jeshi la polisi kwa kazi waliyoifanya kwa mda
mfupi mara baada ya tukio hilo huku kamanda Konyo akiendelea kuwaasa
wananchi wazidi kutoa ushirikiano kwa jeshi la polisi ili kuimarisha
amani katika mkoa huo.

