MAFUNZO YA USIMAMIZI WA SHERIA YA MAZINGIRA NA UDHIBITI WA BIASHARA HARAMU YAFANYIKA ARUSHA

Mkuu wa Wilaya ya Arumeru Bw. Nyirembe Munasa (Kulia) akiongea na mmoja wa washiriki wa mafunzo ya usimamizi wa Sheria ya Mazingira na Udhibiti wa biashara haramu ya bidhaa zinazoharibu tabaka la Ozoni. Katikati ni Kaimu Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Mazingira Bi. Rogathe Kisanga. (Picha Na Lulu Mussa). 
 =======  ===========  =============
 
Imeelezwa kuwa zaidi ya asilimia 90 ya Kemikali zinazoharibu tabaka la Ozoni hutumika katika vipoozi (refrigerants) kama majokofu na viyoyozi na matumizi ya kemikali hizi yapo kwa wingi katika nchi zilizoendelea na zinazoendelea kama Tanzania.

Hayo yamesemwa leo na Mkuu wa Mkoa wa Arusha katika Hotuba iliyosomwa kwa niaba yake na Mkuu wa Wilaya ya Arumeru Bw. Nyirembe Munasa katika ufunguzi wa Mafunzo ya Siku mbili kwa washiriki  kutoka Sekta mbalimbali wakiwemo Maafisa Forodha, Maafisa Biashara, Polisi, Mahakama, Waendesha Mashtaka, Uhamiaji, Wataalamu wa Mazingira na Vyombo vya Habari.

Amesema, tafiti mbalimbali duniani zinaonyesha kuwa mionzi ya kikiukaurujuani (Ultraviolent-B radiation) husababisha kuongezeka kwa magonjwa ya saratani ya ngozi, uharibifu wa macho na upungufu wa uwezo wa mwili kujikinga na maradhi.

Hata hivyo, katika kukabiliana na changamoto za mionzi hiyo mwaka 1993 Serikali  ya Tanzania iliridhia mkataba wa Vienna na Montreal kwa lengo la kudhibiti na kusitisha utengenezaji na matumizi ya kemikali zinazoharibu tabaka hilo kwa awamu kwa kuzingatia upatikanaji mbadala na rafiki kwa Tabaka la Ozoni.

Japokuwa juhudi za kuhamasisha wadau kuhusu faida za kutumia kemikali mbadala na teknolojia mpya katika vifaa na mitambo mbalimbali zimeendeleshwa kwa kipindi kirefu, matumizi ya kemikali haribifu bado yapo. 

Changamoto hii imetokana na kupungua kwa uingizaji wa vifaa hasa majokofu na viyoyozi vilivyotumika na vinavyotumia kemikali zisizo rafiki wa tabaka la Ozoni, uhaba wa mitambo ya kunasa na kurejereza vipoozi katika soko na ongezeko la mafundi wasiokuwa na taaluma na vifaa sahihi vya kuhudumia majokofu na viyoyozi.

Mafunzo haya ya siku mbili yanafanyika katika Chuo cha Utalii Arusha na yanahusisha washiriki kutoka mikoa ya Arusha, Tanga na Kilimanjaro.

Na Lulu Mussa
Afisa Habari
Ofisi ya Makamu wa Rais – Arusha


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo