WAKULIMA WAMBANA "KOO" MKUU WA MKOA

 Simanjiro.
 
WAKULIMA wa Kijiji cha Komolo Wilaya ya Simanjiro Mkoani Manyara wamemlalamikia Mkuu wa Mkoa wa Manyara  kutokana na kitendo cha wafugaji wa eneo hilo kuingiza punda kwenye mashamba yao hivyo kuharibu mazao yao.

Wakiongea   na Mkuu wa mkoa huo Elaston Mbwilo alipotembelea kijiji chao kuhamasisha wananchi wajitokeze kwenye zoezi la sensa ya watu na makazi Agosti 26 mwaka huu walisema punda hao wamewapa hasara kubwa.

Waliongeza kuwa  wamejaribu kufikisha kilio chao kwa uongozi wa eneo hilo ili wafugaji hao wachukuliwe hatua kutokana na kitendo chao cha kuingiza punda kwenye mashamba yao lakini hakuna hatua yoyote wafugaji hao waliyochukuliwa.

Walibainisha kuwa  ipo siku walitaka kuzikata kwa panga punda zilizoingia kwenye mashamba na kuharibu mazao yao lakini waliona jambo hilo ni ukatili na utasababisha vurugu baina ya wakulima na wafugaji wa eneo hilo.

“Hapa kijijini kwetu viongozi hawakai kabisa ofisini yaani kila ukienda ofisini hukuti kiongozi yeyote nashangaa leo hii baada ya kusikia mkuu wa mkoa anatembelea eneo hilo ndiyo wanafika,” alisema mmoja kati ya wakazi hao. 

Aidha akiongea  kuhusu hilo,Mbwilo aliuagiza uongozi wa wilaya hiyo kufuatilia suala hilo kwa kuhakikisha kuwa viongozi wa kijiji hicho wanasimamia zoezi la kukamata mifugo inayoharibu mazao yao na kuwalipa fidia wakulima hao.    

“Hatuwezi kuvumilia hali hii hivyo viongozi wa wilaya kupitia kijiji cha Komolo wahakikishe kuwa mifugo inayokamatwa kwenye mashamba ifidiwe na wafugaji hao ili wakulima wasione kama wanaonewa,” alisisitiza Mbwilo.

Kwa upande wake mkuu wa wilaya ya Simanjiro Kanali Cosmas Kayombo alibainisha kuwa  wakazi wa kijiji hicho pamoja na viongozi wake wanatakiwa watunge sheria ndogo za kuweza kudhibiti uaribifu wa mazao mashambani.

Alisema kuwa watakapokuwa na sheria zao ndogo hapa kijijini kwao zitawasaidia kulipwa fidia na siyo na punda tu hata mifugo mingine ikiharibu mazao watafidiwa pindi watakapozipitisha sheria hizo ndogo.


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo