Kijana aliyetambulika kwa jina la Ahmed Abdalla amejikuta mikononi mwa jeshi la polisi kwa tuhuma za kutoa huduma ya afya kinyume cha sheria na mazingira yasiyo rafiki kwa jamii katika kijiji cha Mapogolo kata ya Milo wilayani Ludewa mkoani Njombe.
Awali jeshi hilo liliweka mtego wa kumkamata katika eneo la nyumba anayofanyia shughuli hizo lakini hawakufanikiwa kumkuta ambapo walibaini kuwa yupo katika kata ya jirani ya Mlangali na polisi walipofika katika kata hiyo walimkuta akiwa baa akinywa pombe ndipo walipo mkamata na kurejea nae katika eneo lake la kazi na kuanza kufanya upekuzi.
Wakati wa mahojiano na Kaimu Mganga mkuu wa wilaya ya Ludewa Leslie Mhagama mtuhumiwa huyo amedai kuwa na elimu ya msalaba mwekundu huku akiomba kutotoa maelezo zaidi mpaka pale atakapofikishwa kituo cha polisi.
Hata hivyo baada ya kukamilisha upekuzi Kaimu Mganga mkuu huyo alieleza vitu mbalimbali vilivyoweza kubainika vikiwemo vifaa vya kutolea mimba na kuunganisha mifupa.
Kaimu kamanda wa Polisi mkoa wa Njombe Butusyo Mwambelo amethibitisha kukamatwa kwa mtuhumiwa huyo kwa hatua zaidi za kisheria huku upelelezi ukiendelea.