Mwanamke mchapakazi aliyeazimia kupata elimu kwa vyovyote vile ameamua kurejea shuleni.
Mama huyo wa watoto saba alijiunga na darasa la 3 katika Shule ya Msingi ya Loikas kaunti ya Samburu ili kuendeleza masomo yake.
Ngelemo Leleruk alisema amerejea shuleni kwani wenzake walikuwa wamesoma na walikuwa na maisha bora. "Wenzangu wamesoma na wako mbele sana kimaisha. Nimekuja kusoma na kupata maarifa kama wao," aliambia Citizen TV Kenya.
Mama huyo mwenye umri wa miaka 31 alinyimwa nafasi ya kusoma akiwa na umri mdogo kutokana na kuolewa akiwa na umri wa miaka 13. Katika miaka yake 18 ya ndoa, amezaa watoto saba ambao anawatunza na mume wake ambaye amemshika mkono.
Mume wa Leleruk, Thomas Leleruk, alionyesha furaha yake na kuunga mkono mpango wa mke wake wa kurejea shuleni. Mwalimu wake, Rose Wamoyo, alimsifu Leleruk, ambaye amewashinda wanafunzi wenzake na zaidi ya miaka 20.
"Ni mwanamke aliye na kiu cha elimu. Anauliza maswali na yuko tayari kusoma," alifichua. Leleruk, ambaye alitumia muda mwingi wa maisha yake kuchunga ng’ombe na kulea watoto wake, aliwahimiza wanawake kutafuta elimu, na kuongeza kuwa alirejea shuleni ili kuboresha maisha ya familia yake. "Napenda kuwasihi wanawake na akina mama, muhimu zaidi, wale ambao wako nyumbani na hawajasoma warudi shuleni na kusoma.
Wapate kazi na hata digrii," alisema. Hadithi ya Leleruk iliwagusa watu wengi mitandaoni huku wakimpongeza kwa hatua yake muhimu.