Watu watatu kati ya sita waliotoweka katika mazingira ya kutatanisha usiku wa kuamkia Ijumaa Aprili 6, 2018 katika Kijiji cha Mitambuuni shehia ya Mtambwe, Mkoa wa Kaskazini Pemba wameonekana alfajiri ya leo Jumapili Aprili 8, 2018.
Wameonekana katika Kijiji cha Mkungu Jimbo la Mtambile wilayani Mkoani.
Kamanda wa polisi Mkoa wa Kusini Pemba, Sheikhan Mohamed Sheikhan amethibitisha kupatikana kwa watu.
Amewataja vijana waliopatikana kuwa ni Said Shanani Mohamed (16), Juma Kombo Fimbo (17) na Abdallah Khamis Abdallah (19).
Imeelezwa vijana hao walionekana alfajiri, wawili kati yao mikononi wakiwa na kamba.
Amesema taarifa zaidi itatolewa baadaye na kamanda wa Mkoa wa Kaskazini ambako ndiko walikotoweka.
“Kwa sasa jeshi linafanya kazi na taarifa rasmi itatolewa kwenu na jamii kwa jumla hapo baadaye,’’amesema kamanda Sheikhan.
Amewataka wananchi kushirikiana na Polisi kwa kutoa taarifa zinazoashiria uhalifu.
