ASHTAKIWA MAHAKAMANI KWA TUHUMA ZA KUCHANA NOTI YA SHILINGI 50

MWANAMUME alijipata taabani Alhamisi alipofikishwa mahakamani kwa kurarua noti mbili za Sh50 baada ya kukosana na kondakta wa matatu kuhusu nauli.
James Munene ambaye ni mhudumu wa bucha mjini Ngong, alikamatwa na polisi kwenye barabara ya Ngong-Nairobi muda mfupi baada ya kisa hicho cha Desemba 15.

Mahakama iliambiwa kuwa alimnyang’anya kondakta Kenneth Thairu noti hizo na kuzirarua jambo ambalo ni kinyume cha sheria za uhalifu nchini.

Shtaka lilieleza kuwa mshtakiwa alikasirika Bw Thairu alipomwambia nauli ilikuwa Sh80 naye akasisitiza angelipa Sh50.

Munene alimrukia na kumnyang’anya noti hizo kisha akazirarua akisema zilikuwa zake na hakuna ambaye angemuuliza chochote.

Hata hivyo, dereva wa matatu aliipeleka katika kizuizi cha polisi wa trafiki kwenye barabara hiyo na mshukiwa akamatwa.

Alikabiliwa na shtaka la pili la kumpiga Bw Thairu mdomoni na kumng’oa jino.

Ilidaiwa kuwa alitenda kosa hilo alipomnyang’anya mlalamishi noti alizorarua.

Hata hivyo, alikanusha shtaka mbele ya Hakimu Mkazi wa Kibera Bryan Khaemba aliyemwachilia kwa dhamana ya Sh30,000 na dhamana sawa.

Hakimu alikataa kumwachilia kwa dhamana ya pesa taslimu akisema kulingana na makosa yanayomkabili anaweza kutoroka.

Kesi hiyo itasikilizwa Machi 19 mwaka ujao.


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo