WAFANYABIASHARA JIJINI DAR WAZIDI KUFANYA BIASHARA ZAO KWENYE MAENEO YASIYORUHUSIWA

ZOEZI la kuondoa wafanyabiashara ndogo katika sehemu mbalimbali jijini Dar es Salaam, imedaiwa haliwezi kufanikiwa kirahisi kutokana na baadhi ya wafanyabiashara hao kugoma kuondoka katika maeneo yasiyoruhusiwa, na kuwa suluhisho pekee ni wao kutafutiwa maeneo mazuri ya kufanyia shughuli hizo. 

Wafanyabiashara hao ambao awali waliondolewa kufanya biashara zao katika maeneo yasiyoruhusiwa na Askari waliokuwa wakisafisha jiji, wameonekana kurudi katika maeneo hayo na kuendelea na shughuli zao kama kawaida  katika maeneo mbalimbali ya jiji hilo. 

Wakizungumza, baadhi yao wamedai kuwa maeneo yaliyotengwa kwa ajili ya wafanyabiashara ni machache hivyo yanachukua wafanyabiashara wachache, jambo ambalo linakuwa vigumu kwao kwani ndiyo sehemu pekee ambayo wanatafutia riziki.

Mmoja wa wafanyabiashara hao, Joseph Alphones, anayefanya shughuli zake katika eneo la Buguruni, alisema kitendo cha wao kuondolewa katika maeneo yaliyokatazwa bila kuonyeshwa maeneo yanayoruhusiwa si sahihi na hivyo kusema wanalazimika kurudi katika maeneo ili kuishinikiza serikali kubadili mawazo iliyotoa hapo awali. 

Naye Sophia Samsoni wa Mwenge, alisema licha ya wao kutegemea maeneo hayo kwa kujipatia riziki, serikali inatakiwa ione umuhimu wa kuongeza maeneo zaidi ambayo wanaweza kufanya biashara zao ili kuepusha wizi na uporaji ulioanza katika maeneo mbalimbali ya jiji hilo kutokana na tamko lililotolewa na baadhi ya vijana kukosa kazi na kuamua kujiingiza katika wizi.

Mfanyabiashara mwingine aliyejitambulisha kwa jina la Mama Asumani, wa Ilala alisema, katika suala hilo linatakiwa kuangaliwa na idara mbalimbali serikalini ili waweze kusaidika badala ya kuwatimua katika maeneo hayo.
 
Kwa upande wake, Afisa Uhusiano wa Manispaa ya Ilala, Tabu Shaibu, amesema hawezi kuzungumzia suala hilo kwamaana yuko safarini kwa sasa hadi atakaporudi, ambapo katika hatua nyingine alisema manispaa hiyo katika kipindi cha mwaka jana ilibaini kuwa wafanyabiashara 21,500 hawana maeneo ya kufanyia biashara.
 
Afisa habari wa Manispaa ya Temeke, Joyce Msumba, alisema manispaa hiyo inatarajia kujenga soko jipya la kisasa lenye hadhi ya wilaya ambalo litatumiwa na wafanyabiashara ndogo na hivyo kutatua kero inayolalamikiwa mara kwa mara.
 
Kumbukumbu zinaonyesha kuwa, utekelezaji wa mpango huo unazingatia sheria ya mipango miji Na. 8 ya mwaka 2007 na sheria ya mazingira Na. 20 ya mwaka 2004 ambapo maeneo yaliyotajwa kutoonekana biashara yeyote ni pamoja na Keko, Sandali, hang’ombe, Kurasini, Mibulani na kata ya Gerezani zote za manispaa ya Temeke.
 
Maeneo mengine ni pamoja na Kisutu, Kivukoni, Upanga Mashariki, Mchafukoge, Kariakoo, Mchikichini, Jangwani, na Upanga Magharibi ambayo yako katika manispaa ya Ilala na kata za Hananasif, Kinondoni, Kigogo, Mzimuni na Magomeni zote za manispaa ya Kinondoni.
 


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo