MKUU WA WILAYA ATUHUMIWA KWA MAUAJI KITETO

MKUU wa Wilaya (DC) ya Kiteto mkoani Manyara, Martha Umbulla, amedaiwa kuwa chanzo cha kuchochea mauaji ya wakulima na wafugaji.

Madai hayo yalitolewa na Naibu Spika wa Bunge, Job Ndugai pamoja na mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema (Chadema) wakidai anaendesha utawala wa kibaguzi.

Akizungumza kwa hasira muda mfupi kabla ya kusitisha Bunge kwa ajili ya mapumziko ya mchana jana, Ndugai alisema mauaji hayo sio ya wakulima na wafungaji, bali ni ya kikabila kama yale ya Rwanda na Burundi.

Kauli ya Ndugai ilifanana na ile ya Lema ambaye alikuwa wa kwanza kuwasha moto kwa kusema mauaji hayo yanatokana na utawala wa kibaguzi unaofanywa na Umbulla ambaye pia ni mbunge wa Viti Maalumu.

Kwa mujibu wa Lema, utawala wa kibaguzi wa DC huyo, hauna tofauti na ule wa Mbunge wa Arumeru Magharibi, Goodluck ole Medeye (CCM).

Alisema kuwa kinachotokea Kiteto na kusababisha wakulima na wafugaji kuuana, ni viongozi kujenga misingi ya ubaguzi ambao unafanywa na watawala wa maeneo husika.

“Ukiona watawala wanaanza kufanya mikutano kwa ajili ya kuwabagua watu, ujue moja kwa moja kuwa hali haiwezi kuwa nzuri na ndiyo maana mauaji yanajitokeza.

“Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa nianze kukupa pole wewe mwenyewe kuwa mpaka jana usiku, nimepigiwa simu kuwa watu wawili ambao ni wakulima wa Kiteto wamekufa, pikipiki 11 na trekta moja vimechomwa moto na wamechoma maduka.

“Kwa sababu hivi karibuni DC alifanya mkutano wa wananchi, akasema kuwa wale wageni wakae kushoto na wenyeji wakae kulia. Ni hatari zaidi katika nchi, ni sawa na kusema kama ni vita na viendelee. Hivyo, suala hilo liangalie kwa makini,” alisema Lema.

Hata hivyo, tuhuma za Lema ziliibua hasira za Medeye na kuomba mwongozo wa spika kwa kuomba kama kuna uwezekano kuwepo kwa daftari la kuwaorodhesha wote ambao wanaonekana kuwa na matatizo ya akili ili wajulikane.

“Godbless Lema, mtoto aliyekulia kwenye gheto kwa sababu ya kutelekezwa na wazazi wake, alipata huruma pale Arusha akapata ubunge, kama wana Arusha wangekuwa na ubaguzi ungepataje ubunge wewe?” alisema Medeye na kutishia kwamba uchaguzi mkuu ujao atagombea ubunge jimbo la Lema kwa sababu ndiko alikozaliwa.

Kauli ya Lema iliungwa mkono na Mbunge wa Gairo, Ahmed Shabiby (CCM), ambaye alisema kuwa kimsingi hawezi kuunga mkono hotuba ya waziri yeyote kwani wengi hawatimizi wajibu wao.
Alisema kuwa imekuwa mazoea kwa mawaziri kufika katika Jimbo la Gairo na kuwaahidi wananchi kuwa watapeleka maji, lakini hakuna kinachofanyika.

Mbali na hilo, alisema kuwa kitendo cha wakulima kuuawa katika eneo la Kiteto, ni kutokana na ubaguzi ambao unafanywa na viongozi kutokana na kuwabagua wakulima na wafugaji, huku wakisingizia kuwa eneo wanalolima ni hifadhi.

Akitoa utetezi wake, Umbulla alisema mkutano alioufanya katika Kijiji cha Kimana wilayani Kiteto ulikuwa ukiwalenga wanakijiji hicho tu.

“Naibu Spika, naomba nimpe taarifa mbunge aliyemaliza kuzungumza, mheshimiwa Lema, kuwa mkutano nilioufanya ulikuwa unalenga wananchi wa Kijiji cha Kimana tu kutokana na wakulima kutoka Kongwa na Chemba kuwa na tabia ya kutuvuruga, na Lema asipende kuingia katika mambo ambayo naye anapenda kutuvuruga,” alieleza Umbulla.

>>>Tanzania daima


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo