MAUAJI LUSHOTO YAMPELEKEA MKUU WA WILAYA KUWAOMBA RADHI WANANCHI

SAKATA  la mauaji ya raia mmoja wilayani Lushoto, aliyeuawa kwa kupigwa risasi na polisi, limechukua sura mpya baada ya wananchi wa Kijiji cha Viti, Kata ya Shume kususia ujumbe  wa viongozi wa dini uliotumwa na Mkuu wa Wilaya hiyo, Majid Mwanga kuwaomba radhi.

Mwananchi huyo, Hamis Seif (25), aliuawa kwa kupigwa risasi na askari sita kutoka Kituo Kikuu cha Polisi wilayani Lushoto, waliovamia kijiji hicho Oktoba 17 mwaka jana katika tukio ambalo hadi sasa limegubikwa na utata.

Katika tukio hilo, Athuman Mgazija alijeruhiwa kwa risasi na askari hao sehemu zake za siri baada ya kufyatuliwa risasi na askari hao.

Wakizungumza kwa masharti ya kutotajwa majina yao kwa sababu za kiusalama, baadhi ya viongozi wa serikali ya kijiji hicho wamedai kuwa ujumbe huo wa mkuu wa wilaya ulitumwa Aprili 15 mwaka huu ukiongozwa na Sheikh Mkuu wa Wilaya ya Lushoto, Sheikh Abbas.

Sheikh Abbas alifuatana na msaidizi wake, Amin Abbas pamoja na Mchungaji P. Shemdolwa wa Kanisa la KKKT Usharika wa Shume na Padri Kika wa Parokia ya Malindi.

Wakiwa kijijini hapo, viongozi hao walifanya kikao cha ndani na baadhi ya viongozi wa kijiji hicho wakiongozwa na mwenyekiti wao, Samwel Shelukindo kilichokuwa na lengo la kufikisha ujumbe wa kuwataka radhi.

Mkuu wa wilaya huyo, hakukiri wala kukanusha kutuma ujumbe huo katika kijiji hicho baada ya kushindwa kujibu maswali aliyotumiwa na mwandishi wa habari hizi kwa njia ya ujumbe mfupi kupitia simu yake ya kiganjani.

Mauaji hayo yalitokea baada ya askari kuvamia nyumba ya mwananchi mmoja, Mohamed Hamis usiku wa saa tano wakidai kutekeleza amri ya Mahakama ya Wilaya ya Korogwe kwa kile walichodai alipuuza wito wa mahakama hiyo katika shauri la madai.

Uchunguzi uliofanywa na  waandishi wa habari za uchunguzi wilayani hapa,  umebaini kuwa pamoja na kwamba sasa imepita miezi saba tangu kutokea kwa mauaji hayo,  tukio hilo limefanywa siri na mamlaka husika, ikiwamo kushindwa kuwawajibisha askari waliohusika na mauaji hayo.

Akizungumza na waandishi wa habari hivi karibuni, Diwani wa Kata ya Shume, Rashird Kisimbo,  amehoji ukimya wa polisi kutowakamata askari hao, huku wakihamishiwa  vituo vingine nje ya Wilaya ya Lushoto.

Alisema wananchi wake wataendelea kuzililia damu za wapendwa wao licha ya serikali kukaa kimya bila kuchukua hatua.

Alidai kuwa kuwahamisha vituo na kuwashusha vyeo askari hao siyo suluhisho na haiondoi uhalisia wa tukio hilo, huku akiutupia mzigo wa lawama uongozi wa Serikali ya Wilaya ya Lushoto kwa kutoingilia kati tukio hilo.

Mashuhuda wa tukio hilo wamedai kuwa baada ya askari hao kuvamia nyumba hiyo, Mohamed Hamis na watoto wake pamoja na mke wake walipiga yowe kuomba msaada wakihisi kuvamiwa na majambazi kwani askari hao hawakuwa na sare.

Chanzo:Tanzania daima


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo