WAANDISHI wa habari nchini wanatarajiwa kuungana na wenzao duniani
katika maadhimisho ya Siku ya Uhuru wa Vyombo vya Habari Duniani (WPFD),
yanayotarajiwa kufanyika Mei 2-3.
Akitangaza sherehe hizo jijini Dar es Salaam, Mwenyekiti wa
Taasisi ya Vyombo vya habari Kusini mwa Jangwa la Sahara (MISA),
Mohammed Tibanyendera, alisema maadhimisho hayo yatakayowashirikisha
washiriki zaidi ya 200 yatafanyika jijini Arusha.
Alisema sababu za maadhimisho hayo kufanyika Arusha ni kupata
mrejesho wa maazimio waliyoyafikia kwa kuyapatia kaulimbiu ya “Mount
Meru Declaration”.
Alibainisha baadhi ya mambo waliyokubaliana katika maadhimisho kama
hayo mwaka jana yaliyozishirikisha nchi jirani, ni pamoja na kuboresha
hali za wanahabari.
Tibanyendera alisema katika sherehe hizo kunatarajiwa kuzinduliwa
machapisho mbalimbali, ikiwamo ripoti ya hali ya vyombo vya habari
Tanzania 2014.
Ripoti nyingine itakuwa utafiti wa vyombo vya habari 2014 na ripoti ya uvunjifu wa uhuru wa vyombo vya habari kwa mwaka 2014.
Alisema katika maadhimisho hayo mgeni rasmi anatarajiwa kuwa aliyekuwa Jaji Mkuu na Mwanasheria, Mark Bomani.
