HABARI KAMILI YA KUKAMATWA MBUNGE JOSHUA NASSARI

NASSARI 
MBUNGE wa Arumeru Mashariki, Joshua Nassari (CHADEMA), jana alishikiliwa kwa zaidi ya saa tatu na Jeshi la Polisi mkoani Arusha kwa tuhuma za kumshambulia kada wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Hussein Warsama.

Nassari anadaiwa kufanya shambulio hilo siku ya uchaguzi mdogo wa udiwani Kata ya Makuyuni, wilayani Monduli.

Mbunge huyo alisema aliripoti Kituo Kikuu cha Polisi Mkoa wa Arusha jana asubuhi akiitikia wito wa Mkuu wa Tathmini na Ufuatiliaji wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai, Kamanda Issaya Mungulu.

Alisema baada ya kufika hapo alishikiliwa na Mkuu wa Upelelezi wa Mkoa (RCO), kwa tuhuma za kushambulia watu wilayani Monduli ambapo pia alikataa kuandika maelezo bila wanasheria wake, Mabere Marando na Tundu Lissu.

Nassari alisema baada ya kukataa kuandika maelezo aliambiwa avue saa na vitu vingine kwa ajili ya kupelekwa rumande lakini hata hivyo baadaye askari walimwambia wanampeleka Monduli.

Aliongeza kuwa hata hivyo zoezi hilo halikufanyika na badala yake walimpa fursa ya dhamana aliyoitimiza. Taarifa za polisi kutoka Ofisi ya Mkuu wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai Mkoa wa Arusha (RCO), Duwan Nyanda, Nassari anadaiwa kumshambulia Warsama Julai 16, mwaka huu, huko Makuyuni.

Hata hivyo jitihada za Tanzania Daima Jumapili, kuzungumza na Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Arusha, Lebaratus Sabas, kuzungumzia jambo hilo hazikufanikiwa kutokana na simu zake kutokuwa na majibu.

Naye RCO Nyanda alikiri Nassari kuripoti kituoni hapo lakini akagoma kulizungumzia suala lake kwa madai si msemaji.

Tanzania Daima Jumapili lilidokezwa kuwa polisi walianza kumtafuta Nassari wiki iliyopita na taarifa za jambo hilo zilipelekwa kwa Mkuu wa Upelelezi Wilaya ya Arumeru.

Nassari alibainisha kuwa Julai 24, Kamishina Isaya Mungulu alimpigia simu na kumtaka afike polisi ambapo walivyokubaliana angekwenda jana.

Source: Tanzania Daima


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo