WANANCHI MAKETE WATAKIWA KUWA NA UKARIBU NA VIONGOZI WALIOWACHAGUA

 Mkuu wa wilaya ya Makete Bi Josephine Matiro akizungumza wakati wa kufungua rasmi mdahalo kuhusu utawala bora uliofanyika leo katika Ukumbi wa SUMASESU Tandala
 Washiriki wa mdahalo huo wakimsikiliza mkuu wa wilaya wakati akifungua mdahalo huo
========
Imeelezwa kuwa maedeleo ya wilaya ya Makete yatazidi kusonga mbele iwapo wananchi watashirikiana na viongozi waliowachagua bila woga pamoja na wananchi kutoa maoni yao kuhusu maendeleo ya maeneo yao kwa kuwa maoni yao ni ya msingi katika shughuli za kimaendeleo

Hayo yamesemwa na mkuu wa wilaya ya Makete Bi Josephine Matiro wakati akifungua mdahalo uliofanyiaka leo katika ukumbi wa SUMASESU Tandala ulioandaliwa na mtandao wa mashirika yasiyo ya kiserikali wilayani Makete(UMANGO) uliokuwa na lengo la kujenga tabia ya wananchi kuzungumza na viongozi waliowachagua na kuwauliza maswali kuhusu maendeleo yao

Bi Matiro amesema endapo wananchi watashirikiana bega kwa bega na viongozi wao kutasaidia kuharakisha shughuli za maendeleo kwa kuwa kiongozi ana wajibu wake katika kuleta maendeleo ya eneo analoliongoza lakini pia mwananchi naye ana wajibu wake katika hilo

“Wananchi naomba mtambue kuwa maendeleo hayawezi kutokea kama hamtatoa mawazo yenu kwa viongozi mliowachagua na kuhudhuria midahalo kama hii ambayo inakupa fursa ya kuuliza swali kwa kiongozi wako, endapo hutafanya hivyo hii itasababisha malalamiko miongoni mwenu na tena mtabakia kulalamika mitaani malalamiko ambayo hayatawafikia viongozi mnaowalaumu

Hali kadhalika katika mdahalo huo Afisa mipango Barton Sinene kutoka halmashauri ya wilaya Makete aliwasilisha taarifa ya utekelezaji wa mipango ya maendeleo katika kipindi cha Julai 2012-Mei 2013 katika wilaya yake kwa niaba ya mkurugenzi mtendaji wa halmashauri bw. Iddi Nganya, ambapo amesema kwa kipindi hiki barabara za wilaya na vijiji zimeendelea kuimarishwa kwa kiwango cha changarawe kutoka kilomita 203 hadi kilomita 228 pamoja na madaraja 54 ya zege yamejengwa

Amesema barabara ya Njombe-Makete imeanza kufanyiwa usanifu lili iweze kujengwa kwa kiwango cha lami ambapo utamalizika Machi 2014 pia usanifu wa kilomita 3 unafanyika barabara ya Makete mjini na unatarajiwa kumalizika Julai mwaka huu, zabuni itatangazwa na ujenzi wa kilomita 1.5 kwa kiwango cha lami utaanza Agosti mwaka huu

Katika mjadala huo uliowapa fursa wananchi waliohudhuria kuuliza maswali kwa viongozi wao, hoja mbalimbali ziliibuka na kujibiwa na viongozi waliofika kushiriki na endapo muuliza swali hakuridhika na majibu alipewa nafasi ya kuuliza tena swali la nyongeza

Mmoja wa washiriki aliyejitambulisha kwa jina la Atilio Sanga ameitaka serikali kuwaambia wananchi wa kata ya Tandala kuwa ni lini umeme utafika katani hapo na kuanza kufanya kazi kwa kuwa zoezi hilo awali lilianza kwa kasi lakini kwa sasa haliendelei na hawafahamu ni nini kinachoendelea kwa kuwa tangu mradi huo usimame hawajataarifiwa sababu

“Mimi ningependa serikali tuweke wazi, maana mradi huu ulianza vizuri lakini kwa hivi sasa umesimama na hatujaambiwa kwa nini, au mnasubiri wakati wa kuelekea uchaguzi muanze kutengeneza ili mpate kura?” alisema Sanga

Akitoa majibu ya swali hilo Mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya ya Makete Mh. Daniel Okoka amesema majibu ya swali hilo pia yalitolewa na diwani wao Mh. Egnatio Mtawa wakati wa ziara ya Katibu mkuu wa CCM aliyoifanya wilayani hapo mwezi uliopita, lakini akarudia kuwa mradi huo umesimama kutokana na hali mbaya ya hewa kwa kuwa mradi huo ulianza kutekelezwa wakati wa masika

Amesema kutokana na kunyesha kwa mvua nyingi, uletaji wa vifaa vya kuendelea na mradi huo ulishindikana kutokana na magari makubwa ya kubeba nguzo kushindwa kufika makete kutokana na uharibifu wa barabara, na pale walipolzimisha kupita gari lilikwama na kuzuia mawasiliano ya barabara ya makete-Njombe kwa siku moja

Okoka amesema wamefuatilia suala hilo na kuahidiwa kuwa mradi huo utaendelea kujengwa kwa kasi baada ya mvua kuisha ambapo wanatarajia mwezi huu ama mwanzoni mwa mwezi ujao mradi huo utaendelea na ujenzi hadi Tandala

Kwa upande wake mwakilishi wa idara ya maendeleo ya jamii Bi. Jackline Mroso amesema halmashauri inatambua na kuthamini jitihada za asasi zizizo za kiserikali za kuleta maendeleo katika wilaya ya makete kwa kuwa suala la maendeleo ni la kushirikiana na ameyasema hayo wakatia akijibu swali lililoulizwa na Mchungaji Adili Pagalo kutoka asasi ya ELCT Makete programu ya pamoja tuwalee aliyeuliza kama serikali inathamini mchango wa asasi zisizo za kiserikali

Naye mwenyekiti wa UMANGO Mchungaji Ezekiel Sanga ameuambia mtandao huu kuwa mdahalo huo ni wa pili kufanyika wilayani hapo, ambapo wanatarajia ndani ya mwaka huu kuendesha midahalo miwili itakayowapa pia fursa wananchi kuchangia


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo