KIJIJI CHA USAGATIKWA WILAYANI MAKETE CHAKUBALI KUCHANGIA MRADI WA TREKTA

Diwani wa kata ya Tandala Mh. Egnatio Mtawa

Wananchi wa kijiji cha Usagatikwa kata ya Tandala wilayani Makete wamekubali kuupokea mradi wa trekta ambalo watalazimika kuchangia kiasi kidogo cha gharama huku serikali ikichangia kiasi kilichosalia

Hayo yamebainika kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika leo kijijini hapo kwa kushirikisha uongozi wa kijiji na diwani wa kata hiyo mh. Egnatio Mtawa

Akizungumza na wakazi hao wa Usagatikwa Mh. Mtawa amesema kwa kawaida sehemu yenye maendeleo lazima kuna kuumia hivyo katika mradi huo wa trekta serikali itachangia shilingi milioni 40 huku milioni 8 zikichangwa na wananchi hao

Amesema endapo kijiji hicho kitapata trekta hilo litakuwa na manufaa makubwa ikiwemo kulima mashamba yao, kusafirisha mazao, shughuli za ujenzi ikiwemo ukarabati wa barabara pamoja na kukodishwa kwenye maeneo mengine na kukiingizia kijiji mapato

Pamoja na hayo Diwani huyo amewasisitizia kamati ya usimamizi wa trekta kuhakikisha inadhibiti mapato na matumizi ya trekta hilo ili wananchi wote wanufaike na mradi huo, hivyo kuwataka wananchi hao wakiongozwa na uongozi wa kijiji kupanga viwango vitakavyochangwa na wananchi hao ili michango hiyo ianze kutolewa mapema

Wakitoa maoni yao wananchi hao wamesema hawaoni ugumu wa kuchangia mradi huo, isipokuwa wanataka serikali ya kijiji kuangalia rasilimali za kijiji walizonazo ili waziuze na kiasi kitakachosalia wananchi ndiyo wachangie ili kuwapunguzia gharama 

“Mimi sina tabu mradi huu tumeupokea kwa mikono miwili, isipokuwa serikali ya kijiji iainishe idadi ya wananchi wa kijiji hiki tugawe tuone kila mwananchi anatakiwa kulipia shilingi ngapi, halafu kijiji hiki kina rasilimali kama mashamba, tuyauze na kama haitatosha kiasi kilichosalia tuchangie sisi wananchi” alisema mkazi mmoja aliyejitambulisha kwa jina la Erick

Kauli hiyo iliungwa mkono na wananchi wote huku diwani wao akiwatahadharisha kutouza rasilimali zote za kijiji na mwishowe kijiji kubaki kitupu

“Wenye maamuzi ya mwisho ni ninyi wananchi, mkitaka kuuza sawa, mkitaka kuchanga sawa, lakini hakikisheni hamuuzi kila kitu mwishowe kijiji kinabaki kitupu watu watatushangaa” alisema Mtawa

Kijiji cha Usagatikwa ni miongoni mwa vijiji viwili vitakavyopatiwa trekta, mradi ambao uliibiliwa na wananchi wenyewe kama njia mojawapo ya kuwasaidia katika kilimo


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo