Na Anna Nkinda – Magu
Jamii imetakiwa kufanya kila
iwezalo ili kuhakikisha kuwa watoto wa kike wanasoma na kupata elimu
bora kwa kufanya hivyo kutawasaidia watoto hao kuweza kupambana na
changamoto mbalimbali zinazowakabili katika maisha yao.
Wito huo umetolewa hivi karibuni
na Mke wa Rais Mama Salma Kikwete wakati akiweka jiwe la msingi la
jengo la Hosteli ya wasichana ya chuo cha sanaa na ufundi Bujora
kilichopo wilayani Magu katika mkoa wa Mwanza.
Mama Kikwete ambaye pia ni
Mwenyekiti wa Taasisi ya Wanawake na Maendeleo (WAMA) alisema kuwa ni
wajibu wa jamii kuwatengenezea watoto mazingira mazuri ya kusoma ikiwa
ni pamoja na kuwajengea Hosteli ambayo itawasaidia kuishi shuleni na
hivyo kuepukana na vishawishi ambavyo vinaweza kuwahatarishia masomo
yao.
“Changamoto katika maisha ya
wanawake ni nyingi lakini tunaweza kuzipunguza na hatimaye kuzitokomeza
kabisa kwa kuwapatia elimu bora watoto wa kike ili waweze kuwa na
ufahamu sahihi wa masuala ya maisha kwa ujumla wake na hatimaye kuwa na
ujasiri wa kupambana nayo”, alisema Mama Kikwete.
Aliendelea kusema kuwa alianzisha
taasisi ya WAMA mwaka 2006 moja ya malengo yake ikiwa ni kumsaidia
mwanamke kielimu na hatimaye aweze kujikwamua kiuchumi. Katika Sekta ya
elimu amekuwa mstari wa mbele kuhakikisha kuwa mtoto wa kike ambaye ni
yatima na anatoka katika mazingira hatarishi anapata elimu sawa na
watoto wengine.
Mama Kikwete pia aliwataka
wanafunzi kusoma kwa bidii hadi kufika elimu ya chuo kikuu na
kujiepusha kushika mambo mawili kwa wakati mmoja ambayo yatawapelekea
kupata maambukizi ya ugonjwa wa Ukimwi na ujauzito na hivyo kutotimiza
ndoto zao kwani tabu wanayoipata leo ni mafanikio ya baadaye.
Akisoma taarifa ya chuo hicho
Mwalimu Lilian Bwire alisema kuwa chuo kilianzishwa mwaka 1973 kikiwa
kinatoa mafunzo ya sanaa na ufundi kwa vijana wa jinsia zote lakini
katika miaka ya mwanzoni ya 2000 chuo kilianza kudorora na hatimaye
kukosa wanafunzi kwa sababu mashirika ya wahisani kutoka nchini Denmark
na Ujerumani yalisitisha msaada na chuo kushindwa kujiendesha kwa vile
asilimia70 ya wanafunzi walisoma bure na asilimia 30 walilipa ada kwa
kiwango cha chini.
Mwalimu Bwire aliendelea kusema
kuwa mwaka 2012 wazo la kukiendesha chuo liliibua kutokana na uhitaji
mkubwa wa vijana wengi wanaomaliza kidato cha nne ambao hawapati nafasi
ya kuendelea na masomo ya juu hasa watoto wa kike na hivi sasa chuo
hicho kina wanafunzi 236 kati ya hao 103 ni wanafunzi wa kike.