MADIWANI MBARALI WAPIGWA MSASA JUU YA USAFI NA MAZINGIRA


Na Ibrahim Yassin, Mbarali

WADAU mbali mbali wakiwemo Madiwani  kutoka Wilayani Mbarali Mkoani Mbeya wamepewa semina elekezi juu ya  kuzingatia uchafuzi wa mazingira ili kuepukana na magonjwa ya kuambukizwa.

Akizungumza jana  wakati wa warsha ya  siku moja ya  uhamasishaji wa maji na usafi wa mazingira iliyofanyika katika ukumbi wa Kiluteli iliyopo wilayani humo, muwezeshaji wa warsha hiyo Afisa afya Mkuu mstaafu Bartholomayo Ngaeje alisema kuwa viongozi hao wanapaswa kuchukuwa hatua madhubuti katika kutoa elimu kwa wananchi ili waweze kutambua umuhimu wa usafi na mazingira.

Ngaeje alisema kuwa iwapo viongozi watawajengea wananchi  hofu ya kuchafua mazingira baadhi ya magonjwa katika jamii yatapungua kwa kiasi kikubwa kwa kuwa magonjwa mengi yanatokana na uchafuzi wa mazingira.

Muwezeshaji huyo alisema kuwa  kuwa hivi sasa kumekuwepo na ongezeko kubwa la watoto mashuleni lakini ongezeko hilo haliendani na idadi ya vyoo vilivyopo kwenye shule hizo  jambo ambalo linahatarisha afya za watoto.

Alisema kuwa katika utafiti uliofanywa mwaka 2009 na Shirika la kimataifa UNICEF kwa wilaya 16 nchini zilibaini kuwa asilimia 20 ya wananfunzi  hutumia tundu moja la  choo kwa wanafunzi 100.

Aliongeza kuwa katika utafiti huo pia ulibaini kuwa asilimia 92 ya shule katika wilaya hizo hakuna huduma ya kunawa maji na usafi wa mazingira na kuongeza kuwa asilimia 60 ya walimu hawajui suala la usafi wa mazingira.

Alisema kuwa kuwepo maji ya kunawa kwenye shule unasaidia kupunguza wadudu ambao wanakuwepo kwenye mikono ambayo ni michafu hivyo kupelekea kupunguza kwa magonjwa kama ya Kuhala, Kichocho, Kifua Kikuu na mengine ya kuambukizwa.

Aidha alisema kuwa idara ya elimu inapaswa kutoa muongozo wa kukagua mazingira ya shule badala ya kuwakagua walimu tu bali hata kufahamu hali ya vyoo na mazingira ya shule, kwa kusaidiana na ma bwana afya.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mbarali Henry Ndingo alisema kuwa elimu walioipata wanapaswa kuipeleka kwa wananchi ili nao waweze kufahamu umuhimu wa kutunza mazingira.

Aliongeza kuwa kila mwanasiasa yeyote anaposimama kwenye majukwa analazimika kuanza kwanza kutoa elimu ya kutunza mazingira na baada ya hapo ndipo aendelee na siasa zake.


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo