Wadau wa vyombo vya habari nchini wamelaani hatua ya kutekwa, kuteswa
na kuuawa kwa wanahabari, huku wakidai kuwa mateso ya Mwenyekiti wa
Jukwaa la Wahariri, Absalom Kibanda, kumetokana na msimamo imara wa
kalamu yake.
Wadau hao wakiongozwa na Chama Cha Wamiliki wa Vyombo vya
Habari nchini (MOAT), Baraza la Habari Tanzania(MCT) na Jukwaa la
Wahariri, Wamesema shambulio lililofanywa dhidi ya Kibanda halikutokana
na kitu kingine chochote, zaidi ya kazi yake ya uandishi wa habari.
Kutokana na hali hiyo, wadau hao wamelichukua suala hilo kuwa ni
shambulizi dhidi ya uhuru wa vyombo vya habari nchini na kuwajengea hofu
wahariri, waandishi na wanaharakati wote ili wasitekeleze wajibu wao
kwa umma.
Wakizungumza kwa kupokezana, wamesema tukio hilo ni mfululizo
wa mashambulizi ya ambayo yamejitokeza kwa vipindi tofauti ikianza kwa
waandishi wa habari wa gazeti la Mwanahalisi, Saed Kubenea na Ndimara
Tegambwage, kutekwa kwa Dk. Steven Ulimboka, kuuawa kwa mwandishi wa
kituo cha Channel Ten, Daudi Mwangosi, na sasa mashambulizi dhidi ya
Kibanda.Wameitaka Serikali kuunda tume huru ya wapelelezi ili
kuchunguza undani wa masuala hayo, kwa kuwa kasi ya uchunguzi wa vyombo
vya usalama hapa nchini hairidhishi na pia baadhi ya watendaji ndani ya
vyombo hivyo wanahusishwa na kadhia hizi
