JAMII INANAFASI KUBWA YA KUOKOA WANAFUNZI WANAOJIHUSISHA NA VITENDO VYA NGONO WILAYANI MAKETE

 OCS Francis Massawe

Jamii imetakiwa kuona umuhimu wa kuwasaidia wanafunzi wanaorubuniwa na watu kujiingiza katika vitendo vya ngono ilihali wao ni wanafunzi na kutoa taarifa hizo kwa vyombo vya usalama ikiwemo polisi ili hatua za kisheria zichukuliwe kwa wahusika

Kauli hiyo imetolewa na mkuu wa kituo cha polisi Matamba wilayani Makete OCS Francis Massawe wakati akizungumza kwenye kikao cha wadau wanaotekeleza mradi wa shule salama unaotekelezwa katika kata ya matamba chini ya shirika la SUMASESU kikao kilichofanyika kwenye ukumbi wa kata hiyo

Bw. Massawe amesema kumeibuka wimbi la watu kujihusisha kimapenzi na wanafunzi huku wengine wakiwatorosha wanafunzi hao kwenda nao Mbeya kufanya starehe huku wengine wakitoka na wanafunzi maeneo mengine ya wilaya ya makete na kuja kukaa nao Matamba na kasha kuwarudisha walikowatoa

“Unakuta wengine wanatoroka na wanafunzi kwenda nao Mbeya na wengine wanatoka maeneo mengine kama makete mjini halafu wanakuja nao hapa Matamba kula raha na ilihali ni wanafunzi” alisema Massawe

Amesema kwa mujibu wa sheria mtu chini ya miaka 18 hana maamuzi na mwili wake hivyo yeyote atakayefanya naye ngono ametenda kosa la jinai ambalo ni ubakaji bila kujali kuwa mtu huyo alikubali mwenyewe kufanya mapenzi na mtu huyo

Massawe amesema kwa kiasi kikubwa jamii inawafahamu watu hao hivyo ushirikiano baina ya wananchi na jeshi la polisi utasaidia kutokomeza hali hiyo inayodidimiza maendeleo wilayani Makete

Katika hatua nyingine mkuu huyo amekemea tabia ya wananchi wanaochochea kukwamishwa kwa shughuli za kimaendeleo na kusema ni kosa la jinai na yeyote atakayehusika hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi yake

Amesema wapo baadhi ya watu kwenye jamii wanapandikiza habari za uongo kuhusu jambo Fulani la kimaendeleo ili jambo hilo lisifanyike na kusema kitendo hicho ni cha uchochezi na yeyote atakayebainika kufanya hivyo atachukuliwa hatua kali za kisheria

Hata hivyo ameitaka jamii kutoa taarifa polisi ikiwemo kuwataja baadhi ya wahalifu waliopo katika jamii kwani wao ndio wanawafahamu zaidi kuliko polisi hivyo hatua hiyo itasaidia kupambana na vitendo vya uhalifu


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo