DKT SHEIN: VITAMBULISHO VYA TAIFA SI SUALA LA KISIASA


Na Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ametoa wito kwa Wanzanzibari kuitumia fursa ya kupata vitambulisho vya Taifa kwani ni haki yao kikatiba na kuachana na propaganda za baadhi ya watu kulihusisha zoezi hilo la Vitambulisho vya Taifa na itikadi za kisiasa. Dk. Shein aliyasema hayo leo huko katika viwanja vya Baraza la Wawakilishi, viliopo Chukwani Mjini wa Zanzibar. Katika Sherehe za utoaji wa Vitambulisho vya Taifa.

Katika maelezo yake, Dk. Shein alirejea kauli yake ya kuwahakikishia wananchi wa Zanzibar kuwa Vitambulisho vya Mzanzibari Mkaazi vitaendelea kuwepo na kutumika kwa madhumuni yaliokusudiwa kwa mujibu wa Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984.

Alisema kuwa uzoefu wa makosa yaliyotokea wakati wa usajili wa Vitambulisho vya Mzanzibari Mkaazi utumike ili kuondoa kasoro na matokeo yatakayoathiri kupatikana ufanisi katika kuendesha zoezi hilo la Vitambulisho vya Taifa.

Alieleza kuwa kuwepo kwa vitambulisho vya Taifa, kutaisaidia Serikali katika kupanua wigo wa ukusanyaji wa mapato yake na hivyo kuweza kuziimarisha huduma za kijamii, kama vile elimu, afya na upatikanaji wa maji safi na salama.

Aidha, alisisitiza kuwa mapato hayo yatasaidia kuimarisha miundombinu ya barabaram huduma za umeme na pia, kuimarisha ulinzi wa raia na mali zao kadhalika itakuwa ni rahisi katika kukabiliana na tatizo la wafanyakazi hewa jambo ambalo hupelekea serikali kupoteza fedha nyingi.

Dk. Shein aliwakumbusha watendaji wa Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA) kuendeleza umakini na uadilifu walio nao, kwa kutambua dhamana kubwa waliyonayo kwa niaba ya Watanzania.

“Kazi yenu inahitaji uzalendo, ustahamilivu na kuweka mbele maslahi ya nchi badala ya maslahi binafsi, jambo ambalo sina shaka mnalielewa vyema na mtalitekeleza, lakini ni wajibu kukumbushana kwani, tunaambiwa kuwa ukumbusho huwafaa walioamini”alisema Dk. Shein.

Aidha, kwa upande wa Zanzibar, Dk. Shein alisema kuwa wananchi wake hawana budi kuzingatia kuwa kutokana na nchi yenyewe ni ya visiwa haiwezi kuhimili ongezeko lkubwa la watu kutokana na rasilimali zilizopo hasa rasilimali ya ardhi.


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo