Serikali
Mkoani Kinondoni imeliagiza Shirika la Maji Safi na Majitaka Jijini Dar
es Salaam Dawasco kuvifungua vioski 19 vya maji ilivyovifunga katika
Jimbo la Ubungo ili kuondoa adha ya maji inayowalikabili wakazi wa eneo
hilo.
Agizo hilo limetolewa Jijini Dar es Salaam leo na Mkuu wa wa Wilaya ya Kinondoni JORDAN RUGIMBANA wakati wa mkutano wa dharura baina yake na Watendaji kutoka Dawasco na Wenyeviti wa Mitaa ndani ya Jimbo hilo ili kujadili mikakati ya upatikanaji wa maji ya uhakika.
Akifafanua RUGIMBANA amesema, licha ya changamoto mbalimbali inayolikabili jimbo hilo, Dawasco inatakiwa kuchukua hatua kwa kuwakamata watu wanaohujumu miundombinu ya maji na kuwafungulia kesi ya uhujumu uchumi.
Awali wakitoa malalamiko yao, baadhi ya Wenyeviti wa Serikali ya Mtaa wa Kwayusufu na Msigani kata ya Msigani Wilayani Kinondoni Bi MARIAM LWENGE na REMSI LUTUMO wameonesha kusikitishwa na upendeleo unaofanywa na watendaji wa Dawasco wakati wa mchakato wa kuwaunganishia maji wateja wa kawaida.
Akijibu tuhuma hizo Afisa Mwendeshaji Mkuu wa Dawasco JASPER KIRANGO amesema wameamua kuvifungia vioski vinavyomilikiwa na watu binafsi ili kuandaa utaratibu utakaotoa fursa kwa wananchi wote kupata huduma ya maji kwa wakati.