JAMII ya
wahadzabe iliyopo eneo la
Bonde la Yaeda Chini Wilayani Mbulu,Mkoani Manyara imejipanga kikamilifu
kuachana na maisha ya uwindaji,kurina asali,kuokota matunda na kugeukia
kilimo
cha chakula.
Aidha kutokana
na hivi sasa kutoweka
kwa wanyamapori hasa nyani pamoja na tembo waliomalizwa na wawindaji
haramu
(majangili) na kutopatikana kwa urahisi kwa matunda ya mibuyu
kumewasababisha
wageukie kwenye kilimo.
Taarifa hiyo
imetolewa na Mkuu wa
wilaya ya Mbulu Anatory Choya wakati akiongea mbele ya jamii hiyo ya
wahadzabe
alisema kuwa wamewapatia majembe 200 kwaajili ya kulima kwa mikono
pamoja na
kilo 500 za mbegu ya mtama kwa ajili ya kilimo.
Mkuu wa wilaya
hiyo aliendelea
kusema kuwa wametekeleza agizo la Rais Jakaya Kikwete alilolitoa
mwishoni mwa
mwaka jana la kubadilisha maisha ya jamii ya wahadzabe kutoka kutegemea
kuokota
matunda,kurina asali na uwindaji hadi kulima.
“Jamani kupitia
kilimo jamii ya
wahadzabe hivi sasa itabadilika kwa kulima chakula chao kuliko
ilivyokuwa hapo
awali na pia baada ya kugawa vifaa hivyo kwenye kata hii ya Yaeda Chini
na
kugeukia kata ya Eshkesh” alisema Choya.
Kwa upande wake
mwenyekiti wa Kijiji
cha Mongoamono kata ya Yaeda chini Gidabodigi Gidahonda ameishukuru
Serikali
kwa kutoa msaada huo kwa jamii hiyo na kuahidi kuutumia vizuri kwa lengo
lilivyokusudiwa.
Aidha aliongeza
kuwa baada ya
serikali kugawa majembe hayo 200 ambapo kila kaya itapata majembe mawili
yaani
baba jembe moja na mama jembe moja watayatumia kwa kulima kwani wanayo
ardhi
kubwa ya kutosha kwa kilimo.
Naye mmoja kati
ya wakazi wa kijiji
cha Mongoamono ambaye ni jamii ya wahadzabe Therathini Nkwemo mwenye
umri wa
miaka 90 amemshukuru mkuu wa wilaya hiyo Choya kwa kuwapatia majembe
kwani
awali aliwapatia chakula kilichowasaidia wakati wa njaa.
“Tunamshukuru
mkuu wa wilaya kwa msaada wake kwetu kwani hivi sasa badala ya sisi
kumiliki
mishale na pinde tutakuwa tunamiliki majembe ambayo yatatusaidia kulima
mashamba na kupata chakula,” alisisitiza Nkwemo.
Nao
baadhi ya wakazi wa mkoa wa Manyara wanasubiri kwa hamu utekelezaji wa
hatua
hiyo ya kujiunga na ukulima kwani mwanzoni mwa mwaka 2,000 baadhi ya
jamii ya
wahadzabe walijengewa nyumba za bati na wakagoma kuzitumia.
Jamii
ya wahadzabe ni miongoni mwa jamii zilizo na idadi ya watu wachache
nchini,kwani kwa mujibu wa sensa ya mwaka 2002 jamii hiyo ilikuwa na
watu
wasiozidi 1,000 na hawana utamaduni wa familia kuzaliana kwa wingi.