BREAKING NEWZ.......MAAFA YA MAPOROMOKO YA UDONGO YAIKUMBA MAKETE

MAKETE                                               12.04.2011

Mawasiliano ya barabara itokayo Makete hadi Njombe yamekatika usiku wa kuamkia leo baada ya maporomoko ya udongo yanayodhaniwa kuwa mfano wa volcano kufukia barabara hiyo eneo la kilanzi kata ya Lupalilo wilayani Makete na kupelekea mawasiliano hayo kukatika kabisa

Kwa mujibu wa watu walioshuhudia wamesema tukio hilo limetokea kati ya saa mbili na saa tatu jana usiku na kusababisha usumbufu mkubwa kwa watumiaji wa barabara hiyo

Udongo huo mbali ya kufunga barabara hiyo pia umefunika milingoti ya miti mikubwa iliyokuwa katika eneo hilo na udongo huo kusambaa eneo kubwa kama vile ulikuwa ukitawanywa na katapila la kutengeneza barabara

Akizungumza katika eneo la tukio leo asubuhi, mkuu wa wilaya ya Makete Mh. Zainab Ahmad Kwikwega amewataka wananchi kuwa na moyo wa subira kwani serikali ipo pamoja nao katika wakati huu mgumu wa kukatika kwa mawasiliano hayo

Aidha amesema jitihada zilizochukuliwa na ofisi yake mpaka sasa ni kutengeneza njia ya dharura ambayo ni kwa ajili ya watu waendao kwa miguu peke yake ambayo itatumika mpaka hapo ufumbuzi utakapopatikana kwani taarifa hizo zimeshafika hadi ngazi ya taifa

Abiria watokao makete-Njombe wanaishia eneo la tukio na kuvuka ng’ambo ya pili ambako wanakuta magari mengine na wanaendelea na safari zao licha ya kupata usumbufu mdogo wa kuvukia ng’ambo ya pili kupitia njia hiyo ya dharura

P.T.O
Katika kuonesha hali ya kuguswa na janga hilo Kaimu mkuu wa mkoa wa Iringa ambaye pia ni mkuu wa mkoa wa Morogoro Kanali Mstaafu Issa Salehe Machibya amefika katika eneo la tukio na kujionea hali ilivyo huku akisomewa taarifa fupi ya tukio hilo na Mkuu wa wilaya ya Makete Mh. Zainab Kwikwega

Akizungumza na wananchi mara baada ya kupokea taarifa hiyo, Kaimu mkuu huyo wa mkoa amesema kutokea kwa maporomoko hayo ni mpango wa MUNGU hivyo wananchi wawe na subira kwani serikali italishughulikia suala hilo haraka iwezekanavyo

Amesema ofisi yake imeshazitoa taarifa hizo ngazi ya taifa na wataalamu watafika mara moja ili kufanya uchunguzi wa kina wa maporomoko hayo ambayo bado yanaumiza vichwa vya watu wengi

Mbali na mkuu wa mkoa pia kamati ya ulinzi na usalama Mkoa wa Iringa nayo imefika ili kujionea hali ilivyo

Kwa mantiki hiyo watumiaji wa barabara ya makete njombe kwa sasa mnataarifiwa kutotumia barabara hiyo na badala yake zitumike barabara mbadala ambayo ni ya Makete – Bulongwa hadi Mbeya au Makete hadi Mfumbi na kutokea Chimala

Tukio hili limegusa hisia za watu wengi kwani inaaminika kuwa miaka ya 90 maporomoko kama hayo yaliwahi kutokea maeneo ya Luwumbu.

TAARIFA ZAIDI UTAJULISHWA KWA KADRI NINAVYOZIDI KUZIPATA!


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo