Kamati ya Ulinzi na Usalama Wilaya ya Bariadi mkoani Simiyu, imekamata kiwanda bandia kilichokuwa kikitengeneza pombe kali katika Mtaa wa Budeka, Kata ya Sima kwenye Halmashauri ya Mji wa Bariadi.
Wahusika wa kiwanda hicho bubu, walikodi moja ya nyumba katika mtaa huo na kuanza kungeneza pombe hiyo ambayo inadaiwa kutokuwa salama kwa walaji.
Taarifa zinaeleza kuwa bidhaa hiyo ilikuwa ikizalishwa kienyeji licha ya kuwa na nembo halali na stika za Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), lakini pia bidhaa hiyo haina tarehe ya kuanza kutumika wala tarehe ya mwisho wa matumizi.
Mbali na hilo pombe hiyo inadaiwa ilikuwa ikitengenezwa kwa kuchanganywa maji na spirit, ambapo wahusika walikuwa wakitafuta chupa tupu za pombe kali na maboksi yenye nembo kisha kufanya mchanganyiko na kuupeleka sokoni.
Akizungumzia tukio hilo, kwa niaba ya Mkuu wa Wilaya, Katibu Tawala Wilaya ya Bariadi, Nichodemus Shirima amesema wamewakamata watu wawili waliokuwa katika kiwanda hicho bubu huku akibainisha kuwa pombe ambayo ilikuwa ikitengenezwa kwenye kiwanda hicho ni hatari kwa walaji.