Watu sita ambao ni watumishi wa serikali ya wilaya ya kiteto Mkoani Manyara Idara ya afya na elimu wamefariki kwa ajali baada ya gari waliyokuwa wamepanda kugongana na gari nyingine aina ya Prado katika eneo la Pori namba moja Kata ya Partimbo Kiteto Mkoani Manyara
Katika ajali hiyo watu wengine watano wamejeruhiwa na wamehamishwa kwenda hospitali ya Mkoa wa Dodoma kwa matibabu zaidi
Mkuu wa Wilaya ya Kiteto Mbaraka Batenga akiwa hospitali ya Kiteto amethibitisha kutokea kwa ajali hiyo.
Amesema ajali hiyo imehusisha gari la wagongwa, Ambulance Kituo cha Afya Sunya lililokuwa limeleta mgonjwa Hospitali ya Wilaya ya Kiteto kwa ajili ya matibabu na wakati likirudi likiwa limebeba watumishi kurejea eneo la kazi Sunya liligongana uso kwa uso na gari dogo aina ya Prado likitokea barabara ya Kilindi Tanga kuja Kiteto.
Batenga amefafanua kuwa, “Gari la kituo cha afya cha Sunya lilikuwa likimpeleka mgonjwa Hospitali na baada ya kumshusha likiwa linarejea bahati mbaya likagonga uso kwa uso na gari aina ya Prado ambayo iliyokuwa ikitokea Kilindi (Tanga), kuja Kibaya (Kiteto).”
Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Kiteto, Pascal Mbota, amesema amepokea miili ya watu wawili waliopoteza maisha na majeruhi kumi na moja.
Kati ya majeruhi hao wanne wamefariki katika harakati za kuwaokoa, watano wamesafirishwa kwenda Hospitali ya Dodoma kwa matibabu na wawili wanaendelea kutibiwa katika hospitali ya Kiteto.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Manyara RPC George Katabazi, amethibitisha ajali hiyo akisema majina ya waliopoteza maisha na waliopelekwa Hospitali ya Mkoa wa Dodoma pamoja na wanaoendelea na matibabu Hospitali ya Kiteyo yatatolewa kesho.
