Familia ya Bi Neema Athumani Mkazi wa Kijiji Cha Minkoto Mkoani Geita imelalamikia kitendo cha kuachiwa kuandaa na kubeba mwili wa mama yao mzazi kupeleka mochwari baada ya Kufariki Dunia katika kituo cha Afya Cha Katoro alipokuwa akipatiwa matibabu.
Wakizungumza nasi ndugu wa Marehemu huyo wamesema aliyefariki ni mama yao mzazi Elizabeth Shija Mwenye umri wa miaka (80) na baada ya umauti huo kumfika wakashangazwa na hatua ya kuambiwa wauandae mwili kisha kuupeleka mochwari wenyewe badala ya kazi hiyo kufanywa na wauguzi wa Kituo hicho.
Nao baadhi ya wanawake walioshuhudia tukio hilo wamesema kitendo hicho siyo cha kiungwana kwa sababu watu waliofiwa hawatakiwi wawajibike kuandaa na kuupeleka mwili mochwari.
Afisa Mtendaji wa Kata ya Katoro Sospiter Mahushi amefika eneo la tukio na kuahidi kufuatilia suala hilo ambalo limezua sintofahamu katika jamii.
Kwa upande wake Mganga Mfawidhi wa Kituo cha Afya Cha Katoro Dr. Sungura amesema kuwa hali hiyo inasababishwa na upungufu wa vitendea kazi, watumishi pamoja na miundombinu ya kituo hicho kuwa siyo Rafiki.
Chanzo; Nuru Fm
