Mbunge Festo Sanga akijibu maswali ya wananchi wake
Na Edwin Moshi, Makete.
Wananchi wa kijiji cha Ikonda Wilayani Makete mkoani Njombe wametakiwa kutoa ushirikiano wa kutosha kwa serikali pale inapoleta miradi mbalimbali ya maendeleo katika kijiji hicho na kutaka nguvu kazi yao ama ushiriki kutoka kwa wananchi
Katika mkutano wa wananchi hao na Mbunge wa jimbo la Makete Festo Sanga leo Oktoba 10, 2022 uliokuwa na lengo la kusikiliza na kutatua kero za wananchi, mkazi wa kijiji hicho Bw. Shaibu Mahenge ameelezea namna wanavyokabiliwa na tatizo la upungufu wa maji na kuomba mbunge awasaidie
Amesema kutokana na ongezeko matumizi katika shule ya sekondari Lupalilo kumepelekea maji yanayofika kijijini hapo kutotosheleza kwa wananchi hivyo kuiomba serikali kupitia kwa mbunge wao kuwasaidia kutoa maji kwenye chanzo kingine walichokiona kinaweza kupelekea ongezeko la maji kijijini hapo
Akijibu kero hiyo Mbunge Sanga amewaambia wananchi hao kwamba atalifikisha suala hilo kwa wakala wa usambazaji maji vijijini (RUWASA) na watakapofika kijijini hapo wawape ushirikiano wanaoutaka ikiwemo kutowagomea na kujitokeza kwa wingi kwenye mikutano ya kijiji
Mbunge amesema dhana iliyojengeka kuwa maji ni ya wananchi sio kweli, bali hiyo ni rasilimali ya umma inayosimamiwa na serikali, na ndiyo maana inahakikisha hayo maji yanatunzwa na kutumiwa kwa utaratibu mzuri hata kama yameletwa na MUNGU
Peter Msigwa, Shaibu Mahenge na Zablon Msigwa ni miongoni mwa wananchi waliopata nafasi ya kuzungumza kwenye mkutano huo na kutoa maoni yao ikiwemo suala la mbolea za ruzuku zinazoendelea kugawiwa kwa wakulima hivi sasa
Katika hatua nyingine mbunge Sanga ameahidi kutoa mifuko 50 ya Saruji kwa ajili ya ujenzi wa Bwalo katika shule ya msingi Ikonda na kuuagiza uongozi wa kijiji hicho kumpa taarifa pale watakapozihitaji