Mbunge Festo Sanga akishirikiana na wananchi kubeba saruji
Na Edwin Moshi, Makete.
Changamoto mbalimbali zinazowakabili wananchi wa kijiji cha Usagatikwa wilayani Makete mkoani Njombe zitaendelea kutatuliwa, hivyo wananchi hawana haja ya kuwa na wasiwasi kuhusu hiloAkizungumza kwenye mkutano na wananchi wa kijiji hicho leo Oktoba 10, 2022 Mbunge wa jimbo la Makete Festo Sanga amesema anafahamu changamoto zao hususan ujenzi wa zahanati wanaoendelea nao hivi sasa, hivyo amewakabidhi mifuko 50 ya saruji aliyowaahidi ili kufanikisha ujenzi huo na kusema watakapomaliza kuitumia atatoa mifuko mingine 50 na kusema ifikapo 2025 mbunge atachaguliwa kwa kazi alizozifanya kwa kipindi cha miaka 5 na sio kwa nguvu ya fedha aliyonayo
Amesema katika zahanati si kwamba ameishia kutoa saruji pekee lakini pia atakwenda kuhangaika kutafuta fedha zingine na endapo atapata atawapelekea na kama akikosa atarudi pia kuwapa taarifa kwa kuwa hizi ni zama za ukweli na uwazi
Amesema wamepewa fedha za ujenzi wa barabara kilomita mbili kwa kiwango cha changarawe na pia wamepeleka ombi maalum kwa ajili ya matengenezo ya barabara ya Usagatikwa hadi Utweve ambayo imekuwa mkombozi kwa wananchi hao hasa wanaojihusisha na shughuli za kilimo kwa kuwa mashamba yao mengi wanatumia barabara hiyo kuyafikia
Abroni Sanga ambaye ni kada wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) amefika katika mkutano huo na hakusita kueleza namna serikali inavyochapa kazi kwa kuwakumbusha viongozi akiwemo Mbunge yale waliyoyaahidi kwa wananchi wayatekeleze na wayaone kwa vitendo na sio maneno, na kuitumia kauli mbiu ya Rais Samia Suluhu Hassan ya "Kazi iendelee" huku mbunge Sanga akimjibu kwa kumwambia kuwa watachapa kazi kweli kweli
Wananchi waliozungumza kwenye mkutano huo mbali na shukrani zao kwa mbunge na serikali kwa ujumla pia wamezungumzia suala la miundombinu chakavu ya maji, kushukuru umeme kuwafikia kijijini hapo na ukosefu wa barabara kwenye vitongoji vingine ambapo Mbunge amesema anazichukua kwa ajili ya kuzipatia ufumbuzi.