Mkuu wa Wilaya ya Makete mkoani Njombe Juma Sweda ameiagiza Kamati ya ujenzi Kituo cha Afya Mbalache kuhakikisha inanunua vifaa vyote muhimu zikiwemo nondo ili kutokwamisha ujenzi wa Kituo cha Afya.
Ametoa agizo hilo akiwa eneo la ujenzi wa Kituo cha Afya Mbalache kukagua na kuona hali ya ujenzi imefikia hatua ipi tangu Serikali ilipotoa fedha miezi miwili iliyopita.
Sweda amesema kutokuwepo kwa vifaa katika eneo la ujenzi kunasababisha kuchelewa kwa ujenzi, hivyo ameitaka kamati ya ujenzi kuhakikisha inanunua vifaa vyote ili kuendana na kasi ya ujenzi kwa mujibu wa mkataba.
“Hapa hakuna nondo kwa mujibu wa fundi, mnakaa wiki nzima bila vifaa hamuoni kama mnachelewesha kazi? Nataka kesho vifaa vyote ambavyo havipo zikiwemo nondo ziwepo hapa ili fundi aendelee na kazi kwa kasi maana mvua nayo imeshaanza kunyesha niwasisitize kamati acheni uzembe”.
Kwa upande wao wananchi waliofika kufanya shughuli ya upangaji tanuri la tofali ili kuzichoma, wameishukuru Serikali kwa kuwapatia fedha za ujenzi wa Kituo hicho na wamesema wapo tayari kuendelea kutoa ushirikiano katika ujenzi huo
“Tunaishukuru Serikali kwa kutupatia fedha, tumeteseka kwa muda mrefu kufuata huduma Ikonda au Wilaya ya Wanging’ombe Kituo cha Afya Kipengere au tufuate huduma Lupila jambo ambalo wanawake wanapohitaji kujifungua wanakumbatana na changamoto kubwa ya gharama na kusafiri umbali mrefu”.
Halmashauri ya Wilaya ya Makete kupitia mapato yake ya ndani imetoa fedha kiasi cha shilingi Milioni 400 kujenga Kituo cha afya Mbalache kwa lengo la kusogeza karibu huduma kwa wananchi wa Kata hiyo yenye vijiji vitatu ambavyo ni Lupombwe, Mbalatse na Kisasatu.