"Wewe Mstaafu unanunua Gari kwa ajili ya Nini?" Walimu Wastaafu Makete waonywa

MAKETE

Walimu waliostaafu 24 mwaka huu wilayani Makete mkoani Njombe wameshauriwa kuwa makini na matumizi ya fedha za mafao wanazozipata kwani zimelenga kuwasaidia baada ya kustaafu

Kauli hiyo imetolewa jana na mgeni rasmi ambaye pia ni Afisa elimu Msingi wilaya ya Makete Anton Mpiluka katika hafla ya kuwakabidhi zawadi ya bati 20 kila mmoja za futi 10 geji 30 wastaafu hao iliyofanyika katika ukumbi wa Spiritual Makete mjini

Mpiluka amesema kwa kuangalia kwa macho fedha za mafao ya kustaafu huonekana ni nyingi lakini linapokuja suala la matumizi yasiyo mazuri fedha hizo hazitoshelezi

Amewataka walimu hao wastafu kuwa karibu na familia zao katika kipindi hiki pamoja na kubuni miradi ambayo wataweza kuimudu kuisimamia na itakuwa na manufaa kwao huku akiongeza kuwa kustaafu kwao kumesababisha upungufu mkubwa wa walimu katika wilaya ya Makete

Akitoa taarifa fupi katika hafla hiyo Katibu wa Chama cha Walimu (CWT) Wilaya ya Makete Mwl Elizabeth Petro ameikumbusha serikali kuendelea kutatua kwa jicho la kipekee changamoto za walimu wastaafu ikiwemo kuchelewesha kuwapatia mafao yao kwa muda mrefu, pamoja na waajiri kushindwa kuwasafirisha makwao pindi wanapostaafu

Kwa upande wake mwenyekiti wa CWT wilaya ya Makete Mwl Thobias Kasambala amewakumbusha walimu kwa ujumla kuzingatia maadili ya taaluma ya ualimu, pamoja na kulipongeza baraza kuu la CWT Taifa kwa kukubali ombi la kuwapa zawadi walimu wastaafu nchini kote ambao ni wanachama wa chama hicho

Baadhi ya wageni waliopata nafasi ya kuzungumza katika hafla hiyo akiwemo mwakilishi wa TSC Orgen Sanga na afisa elimu sekondari wilaya ya Makete Jacob Meena wamewasihi wastaafu hao kutojiingiza katika siasa kama wagombea, pamoja na kutoacha ualimu wao uelee hewani hata kama wameshastaafu wakubali kushauri ama kufundisha kwa kujitolea pale inapobidi

Wastaafu hao wakizungumza na mwandishi wetu wameahidi kuyafanyia kazi yale yote waliyoambiwa ili uwepo wao katika jamii uzidi kuonekana

Jumla ya wastaafu 24 wakiwemo 23 wa shule za msingi na 1 wa shule ya sekondari wamekabidhiwa zawadi hizo ikiwa ni awamu ya pili tangu utaratibu huo uanze kutumika mwaka jana


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo