Uwepo wa tatizo la ukosefu wa maji katika vitongoji vya Singida na Posta
kata ya Tandala wilayani Makete mkoani Njombe limelalamikiwa na wakazi wa
vitongoji hivyo.
Wakizungumza nasi mara baada kumalizika kwa mkutano uliokuwa unajadili
namna gani ya kutatua tatizo hilo, wananchi hao wamesema kuwa ukosefu wa maji
umedumu kwa zaidi ya wiki mbili sasa na kuwapelekea kutumia maji ya mtoni
ambayo si salama kiafya.
Wamesema kuwa katika mkutano huo uliofanyika stendi mpya ya Tandala
wamesikitishwa Na viongozi wa kitongoji na kijiji kushindwa kufika katika
mkutano huo Licha ya taarifa za mkutano huo kuitishwa na viongozi hao
Akijibu tuhuma za kutofika kwenye mkutano huo pamoja na changamoto za maji
mwenyekiti wa kijiji hicho Bw. Andowise Memba amesema ameshindwa kufika kwenye
mkutano huo kutokana na mtendaji wa kijiji kwenda wilayani Makete kikazi na
yeye kulazimika kubaki ofisini kuhudumia wananchi waliokuwa wakihitaji huduma
mbalimbali za kiuongozi.
Kwa upande wake diwani wa kata ya Tandala Mh, Egnatio Mtawa akizungumza na
Green fm kwa njia ya simu amesema yeye kama diwani analijua tatizo hilo na tayari
ameanza kulishughulikia na kilichochelewesha ni mabadiliko ya mfumo wa fedha za
serikali ambapo kwa kuwa huu ni mwaka mpya wa fedha ni lzima kutakuwa na
mabadiliko ya kimfumo huku akiwapa pole wananchi hao.
Na Asukile Mwalwembe
