Polisi mkoani Iringa limesema miongoni mwa mambo ya kujivunia ni pamoja na kufanikiwa kupunguza uharifu wa aina mbalimbali yakiwemo matukio ya kujinyonga ambayo yanatajwa kuwa ni desturi ya kabila la Wahehe.
Ulevi na hasira ni miongoni mwa sababu zinazotajwa kuchangia ongezeko la matukio ya kujinyonga ambayo yanaainishwa kuwa ni aina ya ukatili unaodaiwa kufanywa na baadhi ya wenyeji wa mkoa wa Iringa na hivyo kujinyonga kuchukuliwa kama desturi ya kabila la Wahehe..
Wahehe ni miongoni mwa makabila makubwa nchini Tanzania, kabila linalopatikana kusini mwa Tanzania- na kabila hilo limejizoa umaarufu wa kitaifa na Kimataifa kutokana na historia ya Chifu Mkwawa kiongozi wa Wahehe ambaye naye inadaiwa kuwa alijiua mwenyewe baada ya kukataa kukamatwa na Wajerumani – kitendo alichokipinga – kwani alikiona kama ni fedhea na aibu kwake.
Polisi mkoa wa Iringa, inazungumzia kushamiri kwa matukio hayo ya kujinyonga, ambapo inasema ililazimika kuweka mikakati ya kupunguza wimbi la matukio ya aina hiyo ambayo kila uchwao yalikuwa yakitokea.
Pamoja na kudhibiti matukio ya kujinyonga, Polisi inadai pia kufanikiwa katika uwanja mpana wa kuyakabiri matukio ya aina mbalimbali.
Taarifa hiyo imetolewa katika hafla iliyoandaliwa na Kikosi cha kuzuia ghasia FFU wakati askari wa kikosi hicho cha FFU wakimuaga ACP Ramadhani Mungi- Kamanda wa Polisi mkoa wa Iringa, anayetaraji kuhama siku za hivi karibuni.
Shughuli hii pia imeambatana na gwaride la heshima kama sehemu ya shukrani kwa kamanda huyu kwa ushirikiano mwema wa kufanikisha kuimarisha ulinzi na usalama wa raia na mali zao.