Jeshi la Polisi limewakamata watu 16 akiwamo Mwenyekiti wa CUF Wilaya ya Bukoba kwa madai ya kuhusika
na vitendo vya uchomaji wa makanisa katika maeneo mbalimbali ya Wilaya ya Bukoba.
Watu hao, wakiwamo viongozi na wanachama wa CUF, walikamatwa juzi na kupelekwa katika Kituo Kikuu cha Polisi mkoani Kagera na Kamanda wa Polisi mkoani Kagera,
Augustine Ollomi aliwaeleza waandishi wa habari kuwa
atalitolea ufafanuzi suala hilo leo.
Waliokamatwa katika tukio hilo, ni diwani aliyemaliza muda wake Kata ya Katoro (CUF), Amini Mashaka, Mwenyekiti wa
CUF, Wilaya ya Bukoba Vijijini, Ladslaus Kashonda, Rwegasira
Kashonda, Abdul Dauda, Mwalimu Shakuru Katakweba, Sulaiti
Katima, Mudathiru Rukindo, Hashimu Kanyonyi, Abdul Nkingireha, Sadiq Mustafa, Hassan Bakuza, Suleiman Mfuruki
na mwingine aliyetambulika kwa jina la Jasson.
Mgombea ubunge wa CUF, Jimbo la Bukoba Vijijini, Buberwa
Kaiza alidai kuwa wote waliokamatwa ni viongozi wa chama hicho na wamebambikizwa tuhuma
za kuchoma makanisa na kukamatwa usiku wa kuamukia leo.
Kaiza alisema kwa mtu anayejua mwelekeo wa kampeni za ubunge na udiwani katika kata za
Katoro, Nyakibimbili, Kasharu, Kaibanja na Kishogo atakuwa anafahamu kuwa masuala hayo
yanahusiana na masuala ya kampeni Hofu ya wananchi Wakazi wa Kata za Katoro na Kaibanja ambako yalitokea matukio matatu ya uchomaji wa makanisa usiku wa kuamkia Jumapili, walisema suala hilo limeleta hofu zaidi kwa kuwa hata
kundi lililokuwa linacharaza wananchi na kuharibu mali kabla ya hapo halikuwahi kujulikana,
huku wengine wakisema ni la kisiasa.
Pamoja na matukio ya uchomaji kutokea katika Kata ya Kaibanja, watuhumiwa zaidi ya 15 waliokamatwa wakihusishwa na matukio hayo wote wanatoka kata jirani ya Katoro.
Baadhi ya wananchi wameshangaa kukamatwa kwa mgombea udiwani wa Katoro, Mashaka
akihusishwa na uchomaji wa makanisa wakati amewaongoza kwa vipindi viwili mfululizo sasa.
Mwenyekiti wa Kijiji cha Kaibanja, Muganyizi Bagandanshwa alihusisha vitendo vya uchomaji wa makanisa na kuibuka upya kwa kundi la ‘wakacharaji’.
Bagandanshwa alisema vitu vilivyoteketezwa ndani ya Kanisa la Kiinjili la Kilutheri, Mtaa wa
Kaibanja vina thamani ya zaidi ya Sh2 milioni na vilikusanywa eneo anaposimama kiongozi wa
ibada kabla ya kuteketezwa.
Mchungaji wa Kanisa la Faith Mission lililopo katika Kijiji cha Kaibanja, Laurent Komba alisema
yeye na waumini wake wanaishi kwa hofu wakiamini matukio yaliyotokea kwenye makanisa jirani
yanaweza kuwafikia pia.
Chanzo:Mwananchi
