Mabere Marando yupo hoi Muhimbili

Mwenyekiti wa Chadema Kanda ya Mashariki ambaye pia ni mwanasheria, Mabere Marando amelazwa katika Hospitali ya Taifa Muhimbili juzi jioni akiwa hajitambui. 

Marando ambaye pia ni Mjumbe wa Kamati Kuu ya Chadema, amelazwa katika Jengo la Magonjwa ya Moyo, wodi maalumu ya FF4, chumba namba 2. 

Ofisa Uhusiano wa hospitali hiyo, John Stephen alisema jana kuwa Marando alifikishwa hospitalini hapo juzi jioni akiwa na hali mbaya na kwamba madaktari wanaendelea kumfanyia uchunguzi pamoja na matibabu. 

Alipoulizwa kuhusu tatizo linalomsumbua, Stephen alisema familia imeomba hifadhi kuhusu siri za mgonjwa wao. 

Mwandishi wetu alimtembelea mgonjwa huyo wodini na kushuhudia hali yake huku mama yake mzazi akiwa pembeni, ambaye hata hivyo hakuweza kuzungumza lolote kuhusu hali ya mwanawe. 

Mke wa Marando, Redempta Lyampawe alisema mumewe hasumbuliwi na tatizo la moyo, na kwamba madaktari wameona ni vyema akapumzishwa katika wodi hiyo. 

“Sisi wenyewe hatuongei naye, hawezi kuzungumza wala kufanya lolote, tunafuata ushauri wa daktari kwamba apewe muda wa kupumzika,” alisema Redempta. 

Mkuu wa Kitengo cha Habari na Mawasiliano Chadema, Tumaini Makene alisema chama chake hakina taarifa. 

Chanzo: gazeti mwananchi


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo