Na Eddy Blog
Wananchi wilayani Makete mkoani Njombe wametakiwa kujitokeza kwa wingi kuhakiki taarifa zao katika daftari la kudumu la wapiga kura linalotarajiwa kufanyika wilayani kote kuanzia wiki hii
Akizungumza na mwandishi wa mtandao huu wa edwinmoshi.blogspot.com Afisa Uchaguzi wilaya ya Makete Bw. Gregory Emannuel (pichani juu) amesema zoezi hilo linatarajiwa kuanza Agosti 07-11 mwaka huu na litaendeshwa kwenye ofisi za kila kata ya wilaya ya Makete
Amesema zoezi hilo litawahusu wananchi wote waliojiandikisha katika daftari la kudumu la wapiga kura ambapo wanatakiwa kufika kwenye ofisi za kata yao wakiwa na kitambulisho cha kupigia kura ili wahakiki taarifa zao
Bw. Gregory amesema lengo la serikali kufanya hivyo ni kupata taarifa sahihji na za uhakika na kuwaondoa wale ambao hawana sifa za kuwepo katika daftari hili, pamoja na kurekebisha taarifa kama zilikosewa wakati wa uandikishaji
"Unajua ndugu mwandishi inawezekana mtu aliandikiwa jinsi ya ke ilihali yeye ni mwanaume au aliandikwa me ilihali yeye ni mwanamke sasa hayo ni miongoni mwa mambo ya kurekebisha, cha msingi wananchi wajitokeze kwa wingi" amesema Gregory
Amesema anaomba wananchi wote wa Makete walioandikishwa wafike kwa wingi katika kata zao bila kukosa ili taarifa zao zihakikiwe na wawe tayari kushiriki katika uchaguzi mkuu wa mwaka huu unaotarajiwa kufanyika Oktoba Mwaka huu kwa kuwachagua viongozi wanaowataka