Jamaa huyu kuanza kujichimbia kaburi lake huko Nkasi

Mchoraji maarufu katika Mji wa Namanyere wilayani Nkasi, Gilbert Paul, ambaye alishaanza kujiandalia maziko kwa zaidi ya miaka 15 sasa akiwa hai buheri wa afya, anatarajia kuanza kujichimbia kaburi miezi mitatu ijayo, ili liwe tayari kuhifadhi mwili wake mara mauti yatakapomfika.
Kijana huyo ambaye amekuwa gumzo mjini Namanyere na kwingineko, amedai alianza kujiandalia maziko yake kwa kujichongea msalaba mkubwa na kuusimika juu ya paa la kibanda chake kilichopo katika Mtaa wa Sasala mjini Namanyere.
Msalaba huo mweupe mkubwa umeandikwa tarehe aliyozaliwa Desemba 24, 1977 lakini kufa ameweka alama ya ulizo, huku baadhi ya wageni wanaotembelea mtaa huo wakidhani ni nyumba ya ibada na wengine wakifikiri ni kaburi la mtu mashuhuri.
Wageni wanapoona msalaba huu kwa mara ya kwanza ukiwa umesimikwa juu ya kibanda hicho, hudhani kuwa ni kaburi kubwa alimozikwa mtu maarufu au mtawala maarufu wa kimila, kwani kipo katikati kabisa ya mji huu,“ alisema Jackson Nkwabi mkazi wa mjini humo.
Nkwabi alisema msalaba uliopakwa rangi nyeupe kwa maandishi meusi, umekuwa kivutio cha aina yake kwa wageni wanaofika mjini hapo ambao ni mara yao ya kwanza kuuona.
Akizungumza mjini Namanyere, Paul alisisitiza kuwa msalaba huo ndio utakaosimikwa katika kaburi lake ambalo anatarajia kuanza kulichimba Oktoba mwaka huu.
Alisema yuko katika harakati za kukusanya fedha anazodai kutoka kwa wasitiri wake, ili ifikapo Oktoba mwaka huu, aanze maandalizi ya kuchimba kaburi ambalo atazikwa mauti yatakapomkuta.
“Ningekuwa nimekaribia kuchimba na kusakafia kaburi langu hilo lakini kinachonikwamisha ni baadhi ya wateja niliowafanyia kazi… nawadai hawajanilipa wameniahidi kunilipa baadaye mwezi huu wa Agosti,” alisema.
Hii kazi ya uchimbaji wa kaburi nitaianza Oktoba mwaka huu, ikiwa ni pamoja na kusakafia na kuwekea nakshi…kaburi langu natarajia ligharimu si chini ya Sh milioni moja kisha nitatengeneza jeneza litakalo gharimu zaidi ya Sh milioni moja,” alisema.
Akizungumzia msalaba huo, aliousimika kwenye kibanda chake cha kazi, Paul alisema aliutengeneza mwenyewe kwa gharama ya Sh 40,000.
Paul aliyehitimu kidato cha nne katika Shule ya Sekondari Nkasi mjini Namanyere mwaka 2001, ameoa mke, Paschalia Salvatory (26) na wamejaliwa mtoto wa kike.
Baadhi ya wakazi wa mjini humo na kwingineko wanaamini kuwa Paulo anafahamu siku atakayofikwa na umauti, huku wengine wakimwona amechanganyikiwa, lakini mwenyewe akidai kuwa na akili timamu na kwamba hajui lini atafikwa na mauti na kwamba anaamini ataishi miaka mingi ijayo.


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo