MWENYEKITI wa Baraza la Wanawake Chadema (BAWACHA) na Mbunge wa Kawe,
Halima Mdee (35) na wenzake wanne walisomewa maelezo ya awali jana
katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu ambapo walikubali kuwa wafuasi wa
Chadema na kwamba wanafahamiana.
Mbali na Mdee washitakiwa wengine ni Rose Moshi (45), Renina Peter,
Anna Linjewile (48), Mwanne Kassim (32), Sophia Fanuel (28), Edward
Julius (25) Martha Mtiko (27) na Beaty Mmari (35).
Wakisoma maelezo hayo, Mawakili wa Serikali Ahmed Salim na Wakili
Mwandamizi Tumaini Kweka walidai mbele ya Hakimu Mkazi, Janeth
Kaluyenda, kwamba washitakiwa hao walikamatwa kwa katika Mtaa wa Ufipa
wakiwa wamebeba mabango na kukana mashitaka yote.
Pia walidai kwamba washitakiwa hao walikaidi amri halali ya Polisi
iliyowataka kutawanyika baada ya wafuasi hao kutaka kutembea kwenda
Ofisi ya Rais.
Salim alidai baada ya wafuasi hao kukaidi kufuata amri hiyo, polisi walitumia nguvu kuwatawanya kwa kosa la kufanya fujo.
Wakili wa Utetezi, Peter Kibatala aliiomba mahakama hiyo kufuta
shitaka la pili kwamba washitakiwa hao kwa pamoja walikusanyika kwa
lengo la kutembea kwenye Ofisi ya Rais kwamba shitaka hilo lina
mapungufu kisheria, kwani halikutaja vifungu vya kisheria.
Hata hivyo, upande wa mashitaka ulidai kwamba hakuna madhara yoyote
endapo vifungu hivyo havitatajwa. Kesi itatolewa uamuzi Januari 5
mwakani.