Mwenyekiti wa CUF Profesa Ibrahimu Lipumba.
Na Mwandishi wetu
CHAMA
cha Wananchi (CUF) kinalaani vikali kitendo cha Jeshi la Polisi
kuwapiga Waandishi wa Habari waliokuwa wakifuaitilia kuhojiwa kwa
Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) Freeman Mbowe.
Akizungumza
na waandishi wa Habari katika ofisi za makao makuu ya chama hicho
Mwenyekiti wa CUF Profesa Ibrahimu Lipumba alisema waandishi wa habari
wanahaki za kupata habari lakini cha ajabu Jeshi la Polisi
linawashambuliwa kwa kuwapiga kitendo ambacho ni unyanyasaji hakifai
kufumbiwa macho.
Alisema
pamoja na mapungufu makubwa ya katiba iliyopo Kifungu cha 18 (1) bila
ya kuathiri sheria za nchi, kila mtu yuko huru kutoa maoni yoyote na
kutoa nje mawazo yake, na kutafuta, kupokea na kutoa habari na dhana
zozote kupitia chombo chochote bila ya kujali mipaka ya nchi, na pia ana
uhuru wa mawasiliano yake kutoingiliwa kati.
Alieleza
katika rasimu mpya iliyoandaliwa na Tume ya Jaji Warioba baada ya
kupata maoni ya wananchi inaeleza Uhuru wa habari na vyombo vya habari
katika kifungu cha 31 (1) kinaeleza kila mtu ana haki na uhuru wa
kutafuta, kupata, kutumia na kusambaza habari na taarifa.
Lipumba
alisema katika kifungu hiko pia kinaeleza uhuru wa kuanzisha vyombo vya
habari na njia nyingine za upashanaji wa habari bila kujali mipaka ya
nchi na kwamba vitakuwa huru na haki ya kupata ,kutumia na kusambaza
habari.
Pia
alisema wanachama na wapenzi wa Chadema wana haki ya kujua hatma ya
Mwenyekiti wao kuitwa na kuhojiwa Makao Makuu ya Polisi na kwa hiyo
wangemiminika kwa wingi katika eneo la kuhojiwa.
Alisema
kuwapiga waandishi wa habari makao Makuu ya Jeshi la Polisi kunaonesha
kutojali kabisa haki za binadamu katika nchi yetu. “Katika tukio ambalo
Polisi wanajua linapigwa picha ungetegemea kwamba askari wangejaribu
kulinda taswira ya jeshi la Polisi lisionekane waziwazi kuwa haliheshimu
wala kujali haki za waandishi wa habari kufanya kazi yao. Ikiwa
waandishi wa habari wanaweza kupigwa hadharani, je? Mwananchi wa
kawaida, asiyekuwa na sauti kwenye gazeti wala radio na televisheni
anafanywa nini anapokamatwa na polisi au kubambikiziwa kesi,”alihoji
Lipumba.
Alisema
hilo sio tukio la kwanza la kutumia nguvu kupita kiasi dhidi ya
waandishi wa habari ambapo mwaka jana mwandishi wa Habari wa Channel
10, Daud Mwangosi aliuawa na Polisi kwenye vurugu zilizotokea baada ya
Polisi kuzuia shughuli za kufungua matawi za viongozi na matokeo ya
Polisi aliyeongoza amepandishwa cheo.
Aidha
alisema Jeshi la Polisi kwa kunyanyasa raia wa kawaida pamoja na
waandishi wa habari ,wanasiasa wa vyama vya upinzani ni kutimiza maagizo
ya Waziri Mkuu Mizengo Pinda aliyesema wapigwe tu ,hivyo alisema kwa
kauli zake hizo hana sifa ya kuwa rais.
Alisema
Chadema siyo chama pekee kilichotoa wito wa kufanya maandamano nchi
nzima kuhusu jambo linaloendelea katika Bunge Maalum la Katiba na kwamba
baada ya Rais Kikwete kutoa hotuba ndani ya Bunge Maalum la Katiba
iliyopinga mambo muhimu ya Rasimu ya Katiba iliyowasilishwa na Jaji
Warioba ikiwa ni pamoja na mfumo wa muungano wa serikali tatu na
kushutumu mapendekezo hayo kuwa yatasababisha Jeshi lipindue serikali,
CCM walitangaza kufanya maandamano na mikutano nchi nzima kuunga mkono
hotuba ya Rais Kikwete ambayo ilikuwa na kauli nzito za kichochezi.
Alisema
lengo la kumuhoji Mwenyekiti Mbowe ni kumdhalilisha na kumtisha
asiendelee kutimiza wajibu wake kama kiongozi wa juu wa chama kitendo
hiki ndicho kinachochochea vurugu na fujo hivyo alilitaka jeshi kufanya
kazi kama jeshi na si CCM.
Lipumba
pia alilaani kitendo cha kuwazuia kufanya mikutano katika mikoa ya
Lindi na Mtwara huku viongozi wa CCM wakiwa wanaendelea kufanya mikutano
hiyo.
Hivyo
basi alisema rais Kikwete anapaswa kuwa makini amalize mwaka wake wa
mwisho vizuri na kwamba ubabe wa Polisi wa kuilinda CCM kwa kuzuia
shughuli halali za vyama vya upinzani vitasababisha machafuko nchini.
