DEREVA ASIMULIA JINSI SISTA ALIVYOUAWA KWA KUPIGWA RISASI UBUNGO JIJINI DAR

Mark Mwarabu, dereva aliyekuwa akimwendesha sista wa Kanisa Katoliki, Crecensia  Kapuri aliyeuawa na majambazi wa Kanisa Katoliki, amesema mbinu za kijeshi zilimwokoa katika tukio hilo.
 
Katika tukio hilo, Sista Kapuri kutoka Parokia ya Gaudence-Makoka na ambaye alikuwa mhasibu wa Shule ya Sekondari Mwenyeheri Anuarite kutoka Shirika la Bikira Maria Malkia wa Mitume, aliuawa na majambazi Juni 24 mwaka huu eneo la Riverside, Ubungo jijini hapa alipokuwa akifanya ununuzi katika moja ya duka la chakula.
Akisimulia mkasa huo muda mfupi baada ya kumalizika kwa misa ya kuuaga mwili wa sista huyo tayari kwa safari ya kwenda mkoani Mbeya kwa maziko yatakayofanyika kesho, alisema majambazi hao walipofika hawakuzungumza na mtu bali walifyatua risasi.
“Hawakuzungumza chochote na sisi bali nilisikia mlio wa risasi pekee na kwa kuwa mimi nilikuwa mwanajeshi, nilijua moja kwa moja kuwa hizo ni risasi na nikawaeleza laleni chini (wakiwa ndani ya gari) ili zisiwafike,” alisema.
“Niliposikia hivyo, nilikunja usukani kurudisha gari nyuma wakati huo risasi ziliendelea kufyatuliwa kulenga gari letu na zilikuwa zikitoka katika gari lililokuwa limeegeshwa likishusha mizigo,” alisema Mwarabu aliyedai alistaafu Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) mwaka 1989.
Aliongeza: “Sista aliyekuwa nyuma alifungua mlango na kukimbia ndipo mimi nilipopigwa risasi tatu kwenye mkono wa kulia, mbili zilikata kidole gumba na moja ilinijeruhi kidole cha pete na sasa mkono mzima una ganzi.
“Niliinama kukwepa risasi hizo kwani walikuwa na lengo la kuukata mkono mzima lakini nilikuwa nikikwepa na kuendesha kwa makini na ndipo wakanijeruhi vidole. Namshukuru Mungu kwa kuninusuru.”
Mwarabu alisema wakati majambazi hao wanapiga risasi bila mpangilio, risasi kadhaa zilimpata sista huyo aliyekuwa amebaki ndani ya gari na kupoteza maisha palepale.

 Alisema baada ya hapo wasamaria wema walimuwahishwa Hospitali ya Mwananyamala kwa matibabu na mwili wake ulipelekwa Hospitali ya Taifa Muhimbili.
Kuhusu utata wa fedha zilizoibwa, alisema asingeweza kulizungumzia suala hilo kwa kuwa yeye ni dereva tu.
Juzi Kamanda wa Polisi wa Kanda ya Dar es Salaam, Suleimani Kova alisema fedha zilizoibwa ni Sh20 milioni.
Askofu aelezea kifo
Akihutubia mamia ya waumini waliojitokeza kutoa heshima za mwisho, Askofu wa Jimbo Katoliki la Mpanda, Gerevas Nyaisonga alisema kifo cha Sista Kapuri ni cha kuhuzunisha kutokana na aina ya mauaji aliyofanyiwa.

“Yanayotokea leo matukio kama haya... kwa kuua hatuwezi kuondoa ugumu wa maisha yetu, kwa kuua hatuwezi kuboresha maisha yetu wala kuleta amani,” alisema askofu.
“Sista amefariki, anakwenda kuzikwa na kutuachia maswali magumu yasiyokuwa na majibu. Ukali wa maumivu na mateso angetueleza ni nani aliyetenda hayo,” alisema Askofu Nyaisonga.
Akitoa wasifu mfupi wa marehemu, Mama Mkuu wa Shirika la Bikira Maria Malkia wa Mitume alisema, Sista Kapuri alizaliwa Agosti 29, 1962 na alifunga nadhili zake mwaka 1980.
 Naye askofu msaidizi wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Titus Mdoe akitoa salamu za pole za jimbo hilo na za Baraza la Maaskofu Tanzania (TEC), alisema kifo kimetokea hakuna budi kukipokea.
“Watawa hawa hawana kitu chochote kwani wametoa maisha yao kuitumikia jamii. Ukimwona sista amebeba fuko la fedha siyo lake ni kwa ajili ya kuwahudumia watu.”
Kwa kuwa alikuwa mlezi wa watoto wetu wa taifa la kesho, alikwenda kuwatafutia chakula watoto wake na hao walikuwa wakimsubiri mama yao kuona atakuja na nini, lakini ndiyo hayo yaliyotokea,” alisema Mdoe.
Naye kaimu mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Raymond Moshi alisema Serikali itahakikisha inawatia nguvuni wale wote ambao walijihusisha na tukio hilo. Mushi ambaye pia ni Mkuu wa Wilaya ya Ilala, alisema: “Juhudi siyo kuwapata bali ni kuzuia matukio ya aina hii na tunaomba ushirikiano katika kuwabaini wanaofanya vitendo vya aina hii.”

>>>MWANANCHI


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo