MAMLAKA ya Udhibiti wa Usafiri wa Nchi Kavu na Majini (SUMATRA)
mkoani Lindi, imewataka wamiliki wa Mashua zisizotumia Injini kuacha
kuvusha abiria kwenda ng’ambo ya Bahari, kwa kuwa hali hiyo inahatarisha
maisha ya abiria.
Agizo hilo limetolewa na Mkaguzi wa vyombo vya majini katika mikoa ya Lindi na
Mtwara, Galas Chambo, kufuatia Manahodha wa Mashua hizo kubainika
kuvusha abiria kutoka mji wa Lindi kwenda kwenye eneo la Kitunda katika
Manispaa ya Lindi.
Aidha, amesema vitendo hivyo ni
hatari katika maisha ya wananchi wa eneo hilo na maeneo mengine, kwani
vinaweza kusababisha ajali, kutokana na vyombo vyao kutokuwa na Injini
wala vifaa vya kujiokolea. Amesema
mamlaka hiyo kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi mkoani humo limeanza
kuendesha msako wa kukamata vyombo hivyo, vinavyo kiuka sheria na
taratibu za mamlaka hiyo.
Kwa upande wake mwakilishi wa Jeshi la Polisi mkoani humo, Mkaguzi msaidizi wa Polisi, Baraka Masata, amesema kuwa
Jeshi hilo limeitaka (Sumatra) kutoa elimu kwa wamiliki na Manahodha wa
vyombo hivyo ili waweze kutambua madhara yanayoweza kusababishwa na
vitendo vya kuvusha abiria bila kuwa na vifaa vya usalama.