MAJANGA: POLISI WAKIRI KUMUUA MWANAFUNZI SHULENI KWA KUMPIGA RISASI

 Bw Simon Ndiani ambaye ni babake Isaack Ndiani akiongea na wanahabari nje ya shule ya St Charles Mutego Februari 11, 2014. Picha/ANN KAMONI 

Na OUMA WANZALA

POLISI wamekubali kuwa mwanafunzi aliyekufa katika shule ya St Charles Mutego Education Centre, Lenana, Nairobi,  mnamo Jumapili usiku alipigwa risasi kimakosa na mmoja wao.
OCPD wa Dagoreti Mathew Gwiyo alidai kuwa marehemu aliuawa na polisi waliowafyatulia risasi wavamizi ambao walikuwa wakitoroka.

“Tunachunguza jinsi alivyoweza kuwa miongoni mwa wavamizi hao ndipo akapigwa risasi. Polisi hawakuweza kutambua kuwa alikuwa mwanafunzi kwa sababu hakuwa amevaa sare rasmi za shule bali alikuwa amevaa suruali aina ya jeans,” akasema Bw Gwiyo.

Bw Gwiyo aliongeza kuwa mwanafunzi huyo, ambaye alitambiliwa kama Isaac Lesile, mwenye umri wa miaka 20, alikufa kilomita moja kutoka shuleni.

Mwili wake ulipelekwa katika chumba cha kuhifadhia maiti cha City, Nairobi. Hapo jana, baba yake, Bw Simon Ndiami, alitaka uchunguzi wa kina ufanywe kuhusu kisa hicho alichotaja kuwa cha kusikitisha.

“Sielewi ni kwa nini polisi walimuua mwanangu ambaye alikuwa akiwatoroka wavamizi,” akasema Bw Ndiami. Mwanafunzi huyo wa Kidato cha Kwanza alikuwa amejiunga na shule shule hiyo Jumatano wiki jana. Bw Ndiami alidai kuwa wanafunzi wa shule hiyo walikuwa wamepigana mchana na shambulizi hilo la usiku lilitokana na mzozo huo.

“Ni jambo la kusikitisha sana kwamba mvulana huyo aliuawa na polisi ambao walitazamiwa kumuokoa kutoka kwa shambulizi hilo. Alipigwa risasi kichwani kutoka upande wa nyuma, ishara tosha kwamba alikuwa akitoroka,” akasema mzazi huyo. Mnamo Jumapili watu waliojihami walishambulia shule hiyo mwendo wa saa tano usiku na kuwajeruhi wanafunzi zaidi ya 40. 

Washambuliaji waliingia shuleni baada ya kuvunja ua uliojengwa kwa mbao na kwenda moja kwa moja hadi kwenye mabweni ambako waliwaagiza wanafunzi wote watoke nje.

“Washambuliaji hao ambao walikuwa wamejihami kwa silaha butu walisimama kwenye lango kuu la bweni na kuamuru ufunguliwe kabla ya kutuagiza tutoke nje. Walitumia mbao na mapanga kutupiga mmoja baada ya mwingine,” wanafunzi wakasimulia.

Nyimbo za kivita
Walisema kuwa wakati huo washambuliaji waliimba nyimbo za kivita za jamii ya Wamasaai. Wanafunzi pia walisema washambuliaji hao ambao walikuwa wamefunika nyuso zao, waliwapiga bila huruma ambapo baadhi ya wasichana walizimia.

Mnamo Jumatatu, mwalimu mkuu wa shule hiyo, Bw Bonface Makori ,alidai kuwa baadhi ya wanafunzi waliwasaidia washambuliaji kuingia shuleni.

“Tuko na habari kwamba baadhi ya wanafunzi walijiunga na washambuliaji na hata kuwasaidia kutoroka,” akasema Bw Makori. Aliwakashifu baadhi ya wazazi aliosema hukataa kutoa habari zaidi kuhusu watoto wao wanapotaka wasajiliwe shuleni humo.


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo