HATARI: ARV ZAUZWA OVYO MITAANI HUKO RORYA

Imebainika kuwa dawa za Serikali zikiwamo za kurefusha maisha kwa waathirika wa Ukimwi zinauzwa katika maduka ya dawa baridi na maduka bubu ya watu binafsi katika Wilaya ya Rorya mkoani Mara. 

Uchunguzi wa gazeti hili umebaini kuwa maduka yanayouza dawa hizo mengi yanamilikiwa na watumishi katika vituo vya afya vya Serikali, wakati dawa zinazouzwa ni zile ambazo hutolewa na Serikali kwa ajili ya kupelekwa kwenye Zahanati na Vituo vya Afya kwa ajili ya wagonjwa.

Uchunguzi zaidi umebaini kuwa afya za wanunuzi na watumiaji wa dawa katika maduka husika ziko hatarini kutokana na mazingira yasiyoridhisha ya maduka husika, huku wahudumu au wauzaji katika maduka hayo wakibainika kuwa kuwa si watu wenye elimu ya ufamasia.
Katika Kijiji cha Changuge kata ya Mirare, ilibainika kuwa dawa zikiwamo ARV zinapatikana kwa urahisi katika duka linalomilikiwa na mtumishi anayefahamika kwa jina la Nicolaus Joseph, ambaye ni Muuguzi wa Kituo cha Afya cha Serikali, Changuge.
Uchunguzi huo pia ulibaini kwamba dawa hizo pia zinauzwa katika duka la mtumishi mwingine wa kituo hicho, Pamela Otuma ambalo liko katika Kijiji cha Nyambogo, Kata ya Kitembe Wilayani Rorya.
Hata hivyo, Joseph na Otuma kwa nyakati tofauti walikanusha kuuza dawa za ARV pamoja na nyingine, licha ya kila mmoja wao kukiri kwamba aliwahi kumiliki duka la dawa siku zilizopita.
Joseph alisema duka la dawa alilikuwa akilimiliki lilifungwa Februari mwaka jana baada ya kubainika kwamba kufunguliwa kwake hakukufuata taratibu za kifamasia.
“Nilikuwa na duka ambalo lilikuwa likiniingizia kipato cha ziada, lakini sikuwahi kuuza dawa za Serikali, hata hizo tuhuma zilipotolewa ukaguzi ulifanyika na sikukutwa na dawa zozote kwenye duka,” alisema Joseph na kuongeza:
“Baada ya kufungiwa niliuzwa dawa zilizokuwepo kwa watu wengine wenye maduka na hivi sasa najiandaa kufuata taratibu za kifamasia ili niweze kufungua tena duka langu”. Kwa upande wake Otuma alisema : “Mimi sijawahi kuuza dawa za Serikali katika duka langu, na duka hilo lilikuwa Kijiji cha Nyambogo lakini kulipoanza kuwepo maneno kwamba nauza dawa za Serikali nikalifunga”.
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Rorya, Ephraem Ole Nguyaine alisema malalamiko ya kuuzwa kwa dawa hizo nje ya taratibu yamefika ofisini kwake na kwamba ilikuwa sababu ya kuhamishwa kwa watumishi wa afya akiwamo aliyekuwa Mganga Mkuu wa wa Wilaya hiyo, Daniel Chacha.
“Ninashangaa dawa hizo kudaiwa kuwa bado zinaendelea kuuzwa katika maduka ya mitaani, kwa kweli nitafuatilia zaidi suala hili,” alisema Ole Nguyaine.
Wanaoshi na VVU
Baadhi ya watu wanaoishi na Virusi vya Ukimwi walikiri kununua ARV na dawa nyingine katika maduka hayo ya watu binafsi kutokana na kile walichokieleza kuwa ni uhaba wa dawa hizo katika vituo vya Serikali.

“Nikweli ARV zinauzwa hapa senta ya Changuge kwenye duka la mtumishi wa Kituo cha Afya Changuge watu wananunua pindi dawa hizo zinapokosekana kituo cha afya na dawa hizo gharama yake kwa kopo moja ni kuanzia Sh5, 000,” anasema mmoja wa wagonjwa ambaye aliomba jina lake lihifadhiwe kwa kuofia kwamba huenda akanyanyapaliwa.
Dawa hizo pia zinauzwa katika Mji Mdogo wa Shirati. Mkazi wa Kijiji cha Kyariko, Monika Onyango alisema: “…Ni kweli dawa za ARV wakati mwingine zinapokosekana hospitalini tunazinunua kwenye maduka ya dawa baridi kwa Sh5, 000 kwa kopo moja la vidonge 60”.
Onyango ambaye ni mtumiaji wa dawa hizo aliongeza: “Siwezi kumtaja anayeuza kwa jina au kutaja duka kwa sababu linatusaidia dawa zikikosekana tunazipata huko kwenye maduka binafsi tunaendelea na dozi”
Alisema wao hawajali hata kama wanauziwa dawa hizo na nani, kwani wanachokitaka ni kuhakikisha kwamba afya zao zinaimarika. “Sasa kama dawa zinakosekana hospitali tufanyeje? Inabidi wagonjwa tukatafute kwenye maduka ya dawa kwa pesa zetu...Hizo ndizo changamoto tunazokutana nazo sisi tunaoishi na VVU,” alisema.
Uchunguzi wa gazeti hili umebaini kuwa uuzwaji wa ARV katika maduka ya dawa baridi, unachochewa na sababu mbili kubwa; kwanza ni baadhi ya wagonjwa kukwepa kwenda vituo vya afya, ambako hulazimika kukaa kwenye foleni kwa muda mrefu wakisubiri kupatiwa dawa hizo.
Sababu nyingine ni uhaba wa dawa hizo katika vituo vya afya, hali ambayo kuwalazimisha wagonjwa kwenda katika vituo hivyo mara nyingi kuzifuata, hivyo kuchoka kutokana na baadhi yao kutokuwa na afya nzuri.
Mkazi wa Kijiji cha Changuge, Joice Odello alisema: “Maduka ya dawa baridi yana wateja wa ARV maana mtu akifika tu unahudumiwa mara moja, unatoa pesa unapewa dawa unaondoka zako, lakini ukienda kituo cha afya unatumia muda mwingi kungoja dawa kuna mizunguko mingi wengine ni watu wenye hishima zao hawawezi kupanga foleni na wanaona aibu kujulikana ni wagonjwa.”
Onyango kwa upande wake alisema ukosefu wa ARV ni kero kwao, kwani wakati mwingine zinaweza kupita wiki mbili bila kupata dawa hizo na wakati mwingine hupewa nusu dozi.
Mbali na uhaba wa ARV, pia kumekuwapo na uhaba wa dawa nyingine za magonjwa nyemelezi, hivyo wagonjwa wa VVU wamekuwa wakielekezwa kwenda kununua dawa hizo kwenye maduka binafsi.
Kadhalika agonjwa husika wamekuwa wakilazimika kubeba gharama za vipimo kama vile x-ray ambayo hutozwa Sh15,000 na video Sh30,000.
Mkazi wa Rorya, Adelina Joseph alisema: “Ukimpeleka mgonjwa wa TB gharama ni hizo hizo, ukilazwa unajikuta unalipishwa hata zaidi ya Sh200,000 pamoja na dawa gharama hizo kubwa mgonjwa anakufa, tunaomba wagonjwa wa VVU gharama ziwe chini la sivyo tutazidi kufa”.

CHANZO: MWANANCHI


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo