MTOTO WA MIAKA 13 WILAYANI MAKETE AFARIKI DUNIA BAADA YA KULA MIHOGO ALIYOPEWA NA MAMA YAKE MZAZI


Mtoto Clavery Mbilinyi (13) amefariki dunia baada ya kula mihogo inayodhaniwa kuwa ni ya sumu katika kijiji cha Masisiwe kata ya Ukwama wilayani Makete mkoani Njombe

Akithibitisha kutokea kwa tukio hilo Mratibu mwandamizi wa polisi wilayani Makete ambaye pia ni afisa upelelezi wa wilaya(OCCID) Bw. Gozibeti Komba (pichani) amesema tukio hilo lilitokea saa 2 usiku wa tarehe 23 mwezi huu kijiji hapo

Amesema marehemu Clavery Mbilinyi ni mtoto wa Mama Lezia Elias Sanga ambaye ndiye aliyewaandalia chakula hicho ambapo mara baada ya kula mtoto huyo alianza kulalamika kuwa tumbo linamuuma huku pia wenzake wanne waliokula chakula hicho nao walianza kulalamika kuhusu hali hiyo kwamba na wao wanasumbuliwa na tumbo

Watoto waliodhurika na chakula hicho ni pamoja na Huruma Mbilinyi(13), Alex Mbilinyi(10), Tumaini Mbilinyi pamoja na marehemu na wote walikuwa ni wanafunzi

Komba amesema mara baada ya tukio hilo walipokea taarifa kutoka kwa Afisa mtendaji wa kijiji hicho na ndipo polisi walifika eneo la tukio wakiwa wameongozana na Daktari kutoka hospitali ya wilaya ya Makete ambapo waliweza kupata mabaki ya chakula hicho na kuondoka nayo kwa uchunguzi zaidi

Amesema watoto hao wamelazwa katika hospitali ya consolatha Ikonda na hali zao kwa sasa zinaendelea vizuri

Aidha amesema kwa sasa wao kama jeshi la polisi hawawezi kutolea ufafanuzi kama chakula hicho kilikuwa na sumu au la hivyo wanasubiri taarifa kutoka kwa daktari ndipo maelezo zaidi kuhusu chakula hicho yatatolewa

Na Fadhili Lunati


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo