Mwenyekiti wa Chama cha Kitaifa cha Walimu (KNUT) Wilson Sossion.
WALIMU kote Kenya walipigwa na mshangao Alhamisi walipogundua kwamba walilipwa mshahara wa siku kumi walizofanya kazi Julai.
Walioshtuka zaidi ni walimu walio na mikopo walipokosa pesa baada ya benki kukata malipo ya kila mwezi na kuwaacha mikono mitupu.
“Siwezi nikaamini haya. Sijui nitakavyorudi kazini,” akasema mwalimu aliyevunjika moyo kaunti ya Homa Bay.
Lakini chama cha walimu (Knut), kiliwataka wanachama wake wawe watulivu kikisema walimu watalipwa pesa zilizobaki.
Mwenyekiti wa chama hicho Bw Wilson
Sossion alisema walimu walilipwa mshahara wa siku kumi ambao Tume ya
Mishahara iliagiza kabla ya Rais Uhuru Kenyatta kukutana na maafisa wa
chama hicho na kuagiza walimu walipwe mshahara wote wa Julai.
“Kama chama, tunaitaka Tume ya
kuajiri Walimu (TSC), itume sehemu ya mshahara iliyobaki ili walimu
wapate pesa za kukidhi mahitaji yao ya kifedha,” akasema Bw Sossion.
Alisema kucheleweshwa kwa mishahara kumewatatiza walimu hasa wanaosomea mafunzo mbalimbali.
“Kama alivyoagiza rais, TSC inapasa kulipa walimu mshahara wao waliotolea jasho bila kuchelewa,” akasema Bw Sossion.
Rais Uhuru Kenyatta aliahidi
viongozi wa Knut kwamba walimu watalipwa mshahara wote wa Julai
alipokutana nao Ikulu ya Nairobi wiki jana.
Hii ilikuwa tofauti na msimamo wa
Waziri wa Elimu Profesa Jacob Kaimenyi aliyeshikilia kwamba walimu
watalipwa mshahara wa siku 10 pekee.
Msimamo wa waziri ulipelekea Knut kutisha kuitisha mgomo mwingine ili kushinikiza walimu walipwe mshahara wote.
Ingawa Rais Kenyatta aliingilia
kati na kuidhinisha walipwe mshahara wote, aliwaonya walimu dhidi ya
kukiuka maagizo ya mahakama.
Walimu waliozungumza na Taifa Leo walisema walishtuka kupata pesa chache katika akaunti zao walipoenda kuchukua mshahara wa Julai.
Bi Dorothy Okoth, mwalimu wa shule
ya upili kaunti ya Kisumu alitaja hatua ya TSC kama ukosefu wa uaminifu.
Aliongeza kwamba waliamua kuendelea na kazi licha ya kukosa mshahara.