Na Ibrahim
Yassin,Kyela.
MKAZI wa
kitongoji cha Ndombosya kata ya Itope Wilayani Kyela Mkoani Mbeya Neema Kassika
(37) anashikiliwa na Jeshi la Polisi Wilayani hapa kwa tuhuma za kumuua mtoto
wake wa kiume wa kumzaa aliyejulikana kwa jina la Emmanuel mwenye siku kumi na
moja kwa kumcharanga na mapanga.
Akizungumza
na Blog hii leo Afisa mtendaji wa Kata ya Itope Limi Thomas
alisema kuwa alipewa taarifa za mauaji hayo na Mwenyekiti wa Kijiji hicho cha
Itope juu ya tukio hilo la aina yake lilitokea siku ya tarehe 19/08/2013 ambapo
alifika katika eneo la tukio na kujionea unyama huo.
Alisema
baada ya kupewa taarifa ya uwepo wa viashiria vya mauaji aliamua kuita watu
kadhaa na kuingia ndani ili kujionea ualisia wa mauaji hayo na kwamba baada ya kuona
kuwa mauaji ya mtoto aliyeuawa kwa kucharangwa na mapanga ndipo alipotoa
taarifa kwenye kituo kikuu cha polisi wilaya ambao walifika katika eneo la
tukio.
Alidai kuwa
baada ya polisi kufika katika eneo la tukio wakiwa na daktari waliuchukua mwili
huo na kuufanyia uchunguzi na kuwa mara
baada ya uchunguzi waliruhusu familia ya marehemu kuendelea na mazishi huku
mtuhumiwa akiwekwa lumande na atafikishwa mahakamani mara baada ya uchunguzi
kukamilika.
Aliongeza
kuwa mara baada ya polisi kuondoka walifika maafisa wa kituo chamsaada wa
kisheria kwa wanawake na watoto ambao walitaka kujua tatizo hilo ambapo ofisi
yake iliwapa ushirikiano wa kutosha na kwamba watafanya uchunguzi wa kina
kuhusiana na tukio hilo.
Mkurugenzi
wa kituo cha msaada wa kisheria kwa wanawake na watoto wilayani hapa Kyela
Pallalegal Unity(KYEPU) Annamaria Mirambo alisema kuwa ofisi yake imeyapokea
kwa masikitiko mauaji hayo na kuwa watafanya uchunguzi ili kubaini tatizo
lililopelekea mama huyo kuamua kumuua mtoto wake aliyemzaa mwenyewe na
kuhakikisha kuwa anapelekwa mahakamani ili sheria ifuate mkondo wake.
Baadhi ya
wana Kijiji kwa upande wao mbali na kusikitishwa na uwepo wa tukio hilo pia
walidai kuwa mwanamke huyo anasadikika kuwa anatatizo la ugonjwa wa akili na kuwa huenda
alitenda kosa hilo bila kujijua kutokana na tatizo alilonalo.
