KERO YA MAJI ILIYOKUWA INAIKABILI SHULE YA MSINGI NDULAMO WILAYANI MAKETE YAMALIZIKA


 Kibao cha shule ya msingi Ndulamo.
 Muonekano wa baadhi ya majengo ya shule ya msingi Ndulamo
 Mwalimu mkuu wa shule ya msingi Ndulamo Bosco Godigodi akizungumza na mtandao huu ofisini kwake
 Mwanafunzi Alexander Marko akizungumzia uwepo wa maji shuleni hapo
 Mwanafunzi Timotheo Ibrahim akizungumza na mwandishi wetu
Maji yakitoka kwenye bomba la shule hiyo
========

Kero ya muda mrefu ya ukosefu wa maji katika shule ya msingi Ndulamo wilaya ya Makete mkoani Njombe hatimaye imetatuliwa baada ya idara ya maji wilayani hapo kuamua kutilia mkazo suala hilo

Akizungumza na mtandao huu ofisini kwake mwalimu mkuu wa shule hiyo Bw. Bosco Godigodi Malangalila amesema maji yanapatikana kwa wingi shuleni hapo baada ya kuyakosa kwa kipindi kirefu hali iliyokuwa inaleta picha mbaya shuleni hapo

Amesema tatizo hili limeondoka shuleni hapo baada ya idara ya maji kupeleka mabomba na kuyafunga kufidia yale ya awali yaliyokuwa yakivujisha maji ilihali yalikuwa mapya hali iliyosababisha kijiji cha Ndulamo kukosa maji ikiwemo na shule hiyo

Mwalimu Godigodi amesema awali walifanya maandamano hadi kwenye ofisi za serikali ya kijiji kushinikiza tatizo hilo la maji kuondolewa shuleni hapo na waliohusika na uzembe uliosababisha maji yasifike shuleni hapo wawajibishwe

“Hivi sasa ndugu mwandishi kuna uafadhali mkubwa kwani maji yapo, hata waalimu wanaoishi shuleni hapa wanauwezo wa kulima hata kabustani ka mbogamboga” alisema Mwalimu mkuu huyo

Mwanafunzi aliyejitambulisha kwa jina la Alexander Marko amesema kutokana na maji kutoka shuleni hapo yanawasaidia kunywa maji na kunawa mikono ukizingatia msimu huu ni wa kiangazi

Amesema hivi sasa ile kero ya kwenda kutafuta maji wakati wa masomo na wakati mwingine wanafunzi kuja na maji ya kunywa shuleni kwa sasa haipo kwa kuwa yapo maji ya kutosha

Naye mwanafunzi mwingine Timotheo Ibrahim amesema hivi sasa usafi wa vyoo ni mzuri tofauti na awali lakini pia hata mazingira ya shule yamekuwa masafi kwa kuwa maji hayo hutumia kupigia deki madarasani na vyooni

Katika hatua nyingine mwalimu Godogodi amesema ujenzi wa nyumba ya mwalimu uliokuwa ukamilike mwezi huu, hivi sasa unatarajiwa kukamilika mwezi Septemba mwaka huu kwa kuwa ujenzi huo utaendelea kwa kasi baada ya maji kufika shuleni hapo

Amesema ujenzi huo ulisuasua kutokana na kukosekana kwa maji shuleni hapo lakini kwa kuwa kila kitu cha ujenzi hivi sasa kipo ujenzi huo utakamilika mwezi Septemba


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo