Hatimaye serikali mkoani Mbeya, imevunja ukimya na kuzungumzia hatua
zinazokusudiwa kuchukuliwa dhidi ya uongozi wa shule ya sekondari Forest
ya Jijini Mbeya, wanaodaiwa kutumia moja ya chumba katika ofisi za
shule hiyo kutoa adhabu kwa wanafunzi wanaoshindwa kutoa hongo ya
shilingi 500 hadi 1000 kwa makosa mbalimbali ikiwemo kuchelewa.
Siku ya Jumatatu Taasisi ya kuzuia na kupambana na rushwa nchini
(Takukuru) mkoa wa Mbeya iliwakamata walimu wawili, Faustini Robert na
Josephat Mwasote, kwa tuhuma za kushawishi na kuomba rushwa ya kati ya
shilingi 500 hadi 1000 kwa wanafunzi ambao huchelewa kufika shuleni.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake, Afisa elimu Mkoani
Humo, Juma Kaponda, amesema baada ya serikali kupokea taarifa hizo za
kusikitisha imeanza kufanya uchunguzi wa kubaini ukweli wake ili iweze
kuchukua hatua kali za kukomesha tabia hizo.
Amesema watahakikisha wale wote waliohusika na tuhuma hizo wakiwemo
viongozi wa shule wanachukuliwa hatua kali za kinidhamu kwa kuwa taarifa
zinaonesha tatizo hilo limefanyika kwa muda mrefu shuleni hapo.
Kufuatia tuhuma hizoKaponda amekutana na maofisa elimu wa Jiji la
Mbeya ili kupata taarifa za kina juu ya tukio hilo na kama walikuwa na
taarifa za aina hiyo ambazo ni kinyume na utumishi wa umma.