ZAIDI YA MITI 4000 IMEPANDWA KATA YA TANDALA WILAYANI MAKETE HII LEO


Mgeni rasmi akipanda mti wa uzinduzi

Jumla ya miti ya asili 4,377 ambayo ni rafiki kwa utunzaji wa mazingira ikiwemo vyanzo vya maji imepandwa katika eneo lenye chanzo cha maji cha Ng’wenyo kata ya Tandala wilayani Makete katika uzinduzi wa siku ya upandaji miti kiwilaya

Zoezi hilo limeongozwa na Afisa tawala wilaya ya Makete Bw. Onespholia Mahenge kwa niaba ya mkuu wa wilaya ya Makete Mh. Josephine Matiro ambaye alikuwa mgeni rasmi katika shughuli hiyo

Akizungumza mara baada ya kupanda mti wa ufunguzi Bw. Ngogo amewataka wananchi waliofika eneo hilo kuendelea kupanda miti hiyo katika eneo hilo kwa lengo la kutunza mazingira ya kata hiyo

Amesisitiza kwa kipindi hiki cha masika ni vyema kila mwananchi akapanda miti mingi kadri awezavyo ili kuboresha mazingira ikiwemo kutunza vyanzo vya maji ambavyo kwa kiasi kikubwa vimekuwa vikiharibiwa na watu wachache

Zoezi hilo mbali na kupanda kiasi hicho kikubwa cha miti lakini pia limefanyika zoezi la kuharibu miti ya kigeni ambayo inaharibu vyanzo vya maji ikiwemo mipaini

Kwa upande wake afisa maliasili na mazingira wilaya ya Makete Bw. Uhuru Mwembe amesema wilaya ya Makete imekuwa na utaratibu wa kupanda miti kwa wingi hasa miti ya asili hasa kwenye vyanzo vya maji huku akiutaka uongozi wa kata ya Tandala kuendelea kuitunza miti hiyo iliyopandwa ili iote na kustawi

Amesema katika upandaji huo wa miti miti 2,665 imetolewa na halmashauri ya wilaya ya Makete, miti 1,119 imetolewa na mheshimiwa diwani wa kata ya Tandala Egnatio Mtawa, na miti 521 imetolewa na Udiakonia tandala

Ameitaja aina ya miti iliyopandwa ya kuhifadhi vyanzo ya maji kuwa ni Midobole, mitsalugasi, mitsa, mivengingi, mihove, mienekilunga, milungu na mikuyu

Miti hiyo imepandwa na viongozi kutoka wilayani, shirika la Sumasesu, chuo cha ualimu Tandala, shule ya msingi tandala mazoezi, shule ya sekondari Lupalilo, pamoja na wananchi wa kata ya Tandala


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo