Sakata la
kugundulika
kwa gesi asilia mkoani Mtwara, linazidi kupamba moto baada ya wazee
wanaodai kutoka
mkoani Mtwara kuwasili jijini Dar es Salaam na kutoa tamko wakiitaka
serikali
kuacha mara moja mpango wake wa kuisafirisha gesi hiyo kutoka mjini
Mtwara hadi
jijini Dar es Salaam. Badala yake, wazee
hao kutoka Manispaa ya Mtwara-Mikindani, wametaka kijengwe kituo cha
kusafishia
gesi hiyo mkoani Mtwara.
Akisoma tamko
la wazee hao mbele ya waandishi wa habari jijini Dar es Salaam Suleiman
Mademu,
wazee hao wamesema kuwa, wanawawakilisha wananchi wa mkoa huo pamoja na
vyama
tisa vya siasa vilivyoungana vya ADC, APPT-Maendeleo, Chadema, DP,
NCCR-Mageuzi, Sau, TLP na UDP. Mademu amesema
kuwa, serikali
inafanya kinyume cha ilivyowaahidi wananchi wa Mtwara hapo awali wakati
gesi
hiyo inapogundulika ambapo serikali imeahidi wananchi wa Mtwara watakuwa
wa
kwanza kunufaika na gesi hiyo kwa kujenga kituo cha kuisafisha.
Kutokana na
hali
hiyo, ameunga mkono hatua ya wananchi wa Mtwara kufanya maandamano
Desemba 27,
mwaka jana kupinga gesi hiyo kusafirishwa kwenda Dar es Salaam na kusema
kuwa, maandamano
hayo yamefuata taratibu za nchi na kuwa, hatua hiyo ni moja ya njia za
kufikisha vilio na matatizo yanayowakabili wananchi. Amesema kuwa,
katika
kufanya maandamano hayo, hawakuwa na dhamira mbaya kwani maandamano
yalikuwa ya
amani na yamelenga kufikisha kilio chao serikalini.
Ameongeza kuwa, wanachohitaji
ni vitendo kutawala badala ya ahadi kama ilivyozoeleka nchini huku
akisema
kuwa, wanazo rekodi mbalimbali za kupewa ahadi ambazo hazitekelezeki
ambazo ni kujengewa
barabara, kuwekewa umeme, kuimarishwa kwa bandari, mikopo kwa ajili ya
ujasiriamali na viwanda vidogo kwa ajili ya kubangua korosho.
Katika tamko hilo, wazee hao
wameitaka serikali kuratibu mchakato mzima
wa matumizi ya rasilimali gesi kwa kuishirikisha mikoa ya Kusini kwa
hatua zote
na kwa uwazi na kituo cha kufua umeme kijengwe mjini Mtwara. Aidha
wazee hao wamevitaka vyama vya
siasa kutojitafutia
umaarufu binafsi kwa ajenda hiyo ya gesi, badala yake vishirikiane kwa
njia ya
kuleta maendeleo kwa taifa, kwani kaulimbiu yao ni “gesi kwanza vyama
baadaye.”
Chanzo:The chief
