WAFANYABIASHARA TUNDUMA WACHACHAMAA,WAPINGA KUTOZWA MARA MBILI

Na Ibrahim Yassin, Tunduma
WAFANYABIASHARA wanaosafirisha samaki wakavu na dagaa kwenda nje ya nchi kupitia mpaka wa Tunduma mkoani Mbeya wametishia kufanya maandamano makubwa ya kupinga kitendo cha Serikali kuwatoza ushuru mara mbili katika bidhaa moja.
Wakizungumza na mtandao huu mjini Tunduma, wafanyabiashara hao wamesema kuwa Halmashauri ya Mamlaka ya Mji mdogo wa Tunduma imekuwa ikivunja makubaliano yaliyofikiwa katika vikao vya pamoja na kuanza kuwatoza ushuru mara mbili jambo ambalo linasababisha wateja wao kuwakimbia.
Mmoja wa wafanyabiashara hao, Kijiko Isagaswa alisema kuwa katika makubaliano baina ya wafanyabiashara, Halmashauri na Serikali kuu ni kwamba Bidhaa zote zinazosafirishwa kwenda nje ya nchi zinalipiwa kodi Serikali Kuu katika Wizara ya Maliasili na Utalii na bidhaa zinazouzwa ndani ya nchi ushuru wake unakusanywa na Halmashauri ya Mji mdogo.
Akadai kuwa Halmashauri imekuwa ikikiuka makubaliano hayo na kutaka ikusanye ushuru hata kwa bidhaa zinazosafirishwa nje ya nchi, hali ambayo nasababisha kutoelewana na wafanyabiashara hao, na kusababishwa baadhi yao wasiokubaliana na kitendo hicho kukamatwa na kufunguliwa kesi mahakamani.
Isagaswa alisema kuwa tayari wafanyabiashara wamekaa vikao vya kujadili suala hilo na sasa wameamua kuonana na Mkuu wa Mkoa wa Mbeya ili awasaidie kutatua kero hiyo huku wakidai kuwa kama jitihada hizo zitashindikana watahamasishana kufanya maandamano makubwa mjini Tunduma ili kuishinikiza Serikali iwasikilize.
“Tumeshafanya vikao vingi vya pamoja kujadili suala hili, hata viongozi wa kutoka taifani wamefika hapa tukazungumza na kufikia makubaliano ya Halmashauri ukutojihusisha na ushuru wa bidhaa zinazoenda nje ya nchi lakini imekuwa ikikiuka, sasa tumeamua kuchukua hatua ya mwisho ya kuonana na Mkuu wa Mkoa na ikishindikana tutaandamana ili watusikilize,” alisema Isagaswa.
Mfanyabiashara mwingine, Emmanuel Almasi alisema kuwa wafanyabiashara wanakerwa na kitendo cha kutozwa ushuru mara mbili kwa kuwa kinasababisha bidhaa zao (samaki) wapande bei kiasi cha wateja wao kushindwa kumudu na kuhamia maeneo mengine kama vile Msumbiji, Mwanza na Zanzibar ambako hawatozwi ushuru mara mbili.
Alisema hali hiyo inasababisha bidhaa zao kukosa soko na kuwafanya washindwe kumudu maisha sambamba na kulikosesha taifa mapato halali, kwa kuwa biashara hiyo inakuwa ya kusua sua.
“Kitendo cha kututoza ushuru mara mbili kinatuathiri sana kwa sababu bidhaa zetu sasa hazinunuliki na hivyo kutufanya tuwe na maisha magumu, lakini hata Serikali yenyewe inakosa mapato kwa sababu biashara hii sasa haifanyiki ipasavyo,” alisema Almasi.
Alisema kuwa baada ya wafanyabiashara kulalamika kwa kufuata sheria na taratibu zote bila mafanikio, sasa wako tayari kufanya maandamano ili sauti zao ziweze kusikika kwa viongozi wa kitaifa, ambao wanaamini kuwa huwenda hawajui adha zinazowapata.
Chrispine Simwimba alisema kuwa uvumilivu wa wafanyabiashara dhidi ya manyanyaso ya kukamatwa na kufunguliwa kesi bila sababu za msingi sasa umefikia kikomo na wanachotaka sasa ni kutumia nguvu ya umma kuieleza Serikali kuwa wamechoshwa na unyanyasaji dhidi yao.
“Bidhaa zetu zinakamatwa na kushikiliwa Polisi kwa muda mrefu bila kujali kuwa zinaharibika na kutusababishia hasara, sisi wenyewe tunafunguliwa kesi ambazo hazina hata ushahidi na hivyo kutupotezea muda wa kwenda mahakani kila wakati, haya ni manyanyaso ambayo sasa tunataka uyakomeshje kwa kufanya maandamano makubwa hapa Tunduma,” alisema Simwimba.
Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Abbas Kandoro alipoulizwa kuhusiana na kero ya wafanyabiashara hao alisema kuwa maandamano ni haki ya kikatiba ya kila mwananchi hivyo hatishwi na kauli za maandamo zinazotolewa na wafanyabiashara hao.
Hata hivyo alisema kuwa Serikali imeshatoa maelekezo kwa uongozi wa Halmashauri ya Mamlaka ya Mji mdogo wa Tunduma kuhusu jinsi ya kushughulikia tatizo hilo na anaamini kuwa utekelezaji wa maagizo hao utamaliza tatizo hilo.
“Mamlaka ya mji wa Tunduma tumeshaipatia maelekezo ya kumaliza tatizo hilo hivyo naamini kuwa litakwisha muda si mrefu punde maelekezo yaliyotolewa yatakapoanza kufanyiwa kazi,” alisema Kandoro.
Sakata la wafanyabiashara hao kutozwa ushuru mara mbili liliwahi kufikishwa kwa Mlezi wa Chama Cha Mapinduzi Mkoa wa Mbeya ambaye pia ni Waziri wa Ulizi na Usalama, Shamsi Vuai Nahodha alipofanya ziara ya kichama mkoani hapa hivi karibuni ambaye pia aliagiza Halmashauri ya Mamlaka ya Mji mdogo wa Tunduma kufuata sheria ambayo inaelekeza kuwa bidhaa zinazosafirishwa nje ya nchi zitozwe kodi Serikali Kuu na zile zinazouzwa ndani ya nchi ushuru wake ukusanywe na Halmashauri.


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo